• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
Sibabaishwi na matusi yenu, Uhuru awaambia Tangatanga

Sibabaishwi na matusi yenu, Uhuru awaambia Tangatanga

Na SAMMY WAWERU

RAIS Uhuru Kenyatta Jumatatu amevunja kimya chake kuhusu tetesi za kundi la Tangatanga linalokosoa matamshi yake ‘mamlaka ya urais yanafaa kuwa mikononi mwa jamii tofauti na zile mbili ambazo zimeongoza tangu Kenya ilipopata uhuru’.

Kundi hilo linalohusishwa na Naibu wa Rais, William Ruto limetaja matamshi hayo kama yanayoendeleza ukabila nchini.

Dkt Ruto pia amenukuliwa hadharani akiyakosoa, pamoja na salamu za maridhiano kati ya Rais Kenyatta na kiongozi wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga na Ripoti ya Mpango wa Maridhiano (BBI) inayopendekeza Katiba kufanyiwa marekebisho.

Akiwasuta wanasiasa wa kundi la Tangatanga, Rais Kenyatta alisema hababaishwi na matamshi mazito wanayomrushia.

Kwenye mahojiano ya pamoja na vituo vya redio vinavyopeperusha matangazo yake kwa lugha ya Agikuyu, kiongozi wa nchi Jumatatu alisema kwa sasa haja yake kuu ni kuona amefanyia wananchi maendeleo na kuhakikisha ameafikia sera zake.

“Wanadhani wakinitusi nitawatumia askari washikwe? Kama wameona matusi kwa rais ni bora endeleeni, mimi niko hapa kazi hadi nitakapoikamilisha,” akasema.

Akicharura kundi la Tangatanga, Rais Kenyatta alilionya kutojaribu kusimamisha utendakazi wake wala kuzua fujo nchini.

“Hata kabla hawajaongea na kunitukana, huanza kwa kueleza maendeleo yaliyofanywa. Unadhani hiyo kazi hujifanya? Hufanywa na serikali ambayo ninaiongoza,” Rais akasema.

Akieleza kushangazwa kwake na tetesi za wakosoaji wake, Rais alisema hana shida na yeyote, lengo lake likiwa kuafikia ahadi zake kwa Wakenya kabla kukamilisha hatamu yake ya uongozi 2022.

“Lazima nifanye kazi niliyoahidi wananchi na niikamilishe…kauli yangu kuhusu jamii zingine zipokezwe mamlaka hakuna mahali nimesema ni vita ya 2022, haja yangu ni amani, utulivu na maendeleo ya Kenya,” Rais Kenyatta akafafanua, akiridhia salamu za maridhiano kati yake na kiongozi wa ODM, Raila Odinga, Handisheki, kwa kile alitaja kama “hatua iliyochangia kuleta amani nchini”.

Rais pia aliendelea kuhimiza Wakenya kukumbatia Ripoti ya Mpango wa Maridhiano, BBI, akisema itasaidia kuangazia tofauti zinazojiri kila miaka ya chaguzi, ikiwa ni pamoja na kuleta maendeleo.

BBI inapendekeza kufanyiwa marekebisho ya Katiba, suala ambalo limeonekana kupingwa na Dkt Ruto na wandani wake.

Naibu wa Rais pia amekuwa akikosoa uhalisia wa Handisheki, akihoji inalenga kuzima ndoto zake kuingia Ikulu 2022.

You can share this post!

Wanafunzi wa elimu ya msingi waanza mitihani ya majaribio

Amerika sasa yataka jopo libuniwe kuchunguza matokeo ya...