• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Amerika sasa yataka jopo libuniwe kuchunguza matokeo ya uchaguzi wa Uganda

Amerika sasa yataka jopo libuniwe kuchunguza matokeo ya uchaguzi wa Uganda

IRENE ABALO OTTO na ANDREW BAGALA

AMERIKA sasa inataka tume huru ya uchaguzi nchini Uganda kukagua matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika wiki iliyopita, huku ikisema kuwa imepokea ripoti kuhusu kuwepo kwa visa vya udanganyifu na vurugu.

Tume ya Uchaguzi (EC) Jumamosi ilimtangaza Rais Yoweri Kaguta Museveni, 76, wa chama cha National Resistance Movement (NRM) kuwa mshindi wa uchaguzi huo baada ya kupata asilimia 58.6 ya kura zilizopigwa.Rais Museveni ambaye amekuwa mamlakani tangu 1986 sasa ataongoza nchi hiyo kwa muhula wa sita.

Shughuli ya kupiga na kuhesabu kura ilifanyika ‘gizani’ baada ya serikali kuzima intaneti na kuzuia kutuma au kupokea fedha kwa njia ya simu.

Kupitia taarifa yake iliyotolewa wikendi, msemaji wa wizara ya Masuala ya Kigeni ya Amerika, Morgan Ortagus, alisema kuwa: “Tumeshtushwa mno na ripoti za kuaminika kwamba maafisa wa usalama walisababisha vurugu kabla ya uchaguzi na kulikuwa na visa vya udanganyifu siku ya kupiga kura.”

“Tunahimiza serikali kubuni jopokazi huru ambalo litachunguza ripoti hizo na waliohusika na vurugu hizo wachukuliwe hatua,” akasema Ortagus.

Amerika ilishutumu serikali ya Uganda kwa kuhangaisha wawaniaji wa urais wa upinzani na kugandamiza wanaharakati na mashirika ya kijamii.

“Serikali ya Uganda inastahili kuheshimu haki za kibinadamu za wawaniaji wa urais, ikiwemo haki ya kujieleza,” akasema Ortagus.

Siku ya kupiga kura, maafisa wa usalama wa Uganda walivamia kituo cha kujumlisha matokeo kilichowekwa na mashirika ya kijamii katika Hoteli ya Africana jijini Kampala.

Polisi walikamata maafisa 35 wa mashirika ya kijamii kwa madai ya kuendesha kituo sambamba cha kujumlisha matokeo bila kibali.

Wiki mbili kabla ya uchaguzi mkuu, serikali ilifunga akaunti za benki za baadhi ya mashirika ya kijamii, zikiwemo akaunti za Muungano wa Mashirika ya Kijamii nchini Uganda.Serikali ilidai kuwa mashirika hayo yalikuwa yakifadhili shughuli za ugaidi nchini humo.

Amerika ambayo hutoa msaada wa dola bilioni 1 (Sh100 bilioni) kwa Uganda kila mwaka, ililitaka taifa hilo la Afrika Mashariki kuheshimu demokrasia.

Wawaniaji wa urais walionyanyaswa na maafisa wa usalama ni Robert Kyagulanyi, maarufu Bobi Wine wa chama cha National Unity Platform (NUP) na Patrick Oboi Amuriat wa chama cha Forum for Democratic Change (FDC) ambao waliibuka katika nafasi ya pili na tatu mtawalia, kulingana na matokeo ya EC yaliyotolewa Jumamosi.

Bobi Wine amekuwa akizuiliwa na maafisa wa usalama nyumbani kwake tangu Alhamisi wiki iliyopita. Wakati huo huo, vijana 60 walikamatwa mjini Nsangi wilaya ya Wakiso, baada ya kuandamana kufuatia habari feki kwamba mbunge wa Mityana Municipality Francis Zaake wa chama cha NUP aliuawa kwa kupigwa risasi.Kulingana na polisi, vijana hao walishambulia basi kwa kutumia mabomu ya petroli.

You can share this post!

Sibabaishwi na matusi yenu, Uhuru awaambia Tangatanga

Majangili wazingira wabunge na wanahabari Kapedo