• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
Tangatanga watimua wahubiri na kuteka mazishi ya diwani

Tangatanga watimua wahubiri na kuteka mazishi ya diwani

Na WAIKWA MAINA

MAZISHI ya diwani Mburu Githinji wa wadi ya Rurii, Kaunti ya Nyandarua, Jumanne yaligeuka kuwa uwanja wa fujo baada ya wandani wa Naibu Rais William Ruto kuvuruga ratiba na kuanza kumshambulia Rais Uhuru Kenyatta.

Wanasiasa hao walitwaa ratiba na uendeshaji wa mazishi hayo kutoka kwa viongozi wa makanisa kwa nguvu, ambapo waliendeleza harakati za kuipinga ripoti ya Mpango wa Maridhiano (BBI), huku pia wakizindua kampeni za kuwapigia debe watu wanaopanga kuwania nyadhifa mbalimbali kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Kizaazaa kilianza wakati Mwakilishi wa Wanawake katika kaunti hiyo, Bi Faith Gitau (pichani juu), alipoalikwa kuwahutubia waombolezaji. Kwenye hotuba yake, Bi Gitau alisisitiza lazima wanasiasa alioandamana nao wapewe nafasi kuhutubu pia.

Mapema wiki hii, wahubiri katika kaunti hiyo walikuwa wametangaza kuwa wanasiasa hawataruhusiwa tena kuhutubu katika hafla zinazoongozwa na kanisa.

Juhudi za viongozi wa kanisa kumrai Bi Gitau kuzingatia mpangilio wa ratiba hazikuzaa matunda baada ya mbunge huyo kusisitiza kuwa lazima wageni pia wahutubu.

Katika kile kilionekana kuwa njama iliyopangwa awali, vijana walevi walielekea kwenye jukwaa na kuanza kuwapigia kelele viongozi wa dini huku wakitishia kuvuruga mazishi hayo.

Polisi walikuwa na wakati mgumu kuwakabili vijana hao, ambao walifanikiwa kwenda kwenye jukwaa na kuanza kuondoa vipaza sauti.

Katika ishara nyingine iliyoonyesha kisa hicho kilikuwa kimepangwa, mbunge wa Olkalou, David Kiaraho alinyakua kipaza sauti kimoja na kusimamia hafla.

Bw Kiaraho alianza kuwaita wanasiasa waliokuwepo kuhutubu huku vijana wakishangilia. Vijana hao wanadaiwa kusafirishwa kutoka miji ya Kinangop, Naivasha na Ol Kalou.

Wanasiasa waliohutubu walimuunga mkono aliyekuwa mbunge wa Embakasi ya Kati, John Ndirangu kuwania ubunge katika eneo hilo.

Kwa pamoja, wanasiasa kutoka mirengo yote miwili walimuunga mkono mwanawe marehemu, Bi Mary Githinji kumrithi babake kwenye uchaguzi mdogo utakaofanyika.

Wabunge Rigathi Gachagua (Mathira), Gathiru Mwangi (Embakasi ya Kati) na Bw Kipkirui Chepkwony kutoka Baraza la Maspika wa Kaunti (CAF) walimpigia debe Dkt Ruto.

huku wakimkashifu Rais Kenyatta, handisheki na BBI.

“Tunaambiwa nchi itakumbwa na mapigano ikiwa tutajadili na kupigia debe siasa za ‘wilbaro’, kupinga BBI au kuzungumza kuhusu njama za mabwanyenye na maslahi ya watu maskini. Hatutatishwa! Tunahitaji kueleza ukweli, BBI si suala muhimu katika eneo la Kati na nchi nzima kwa jumla,” akasema Bw Gachagua.

You can share this post!

Wanajeshi wa Uganda wamzima balozi wa Amerika kumtembelea...

K’Osewe alidai nilichovya asali ya mkewe, mshtakiwa...