• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:23 PM
ODM wajuta kuingia katika handisheki bila utaratibu

ODM wajuta kuingia katika handisheki bila utaratibu

LEONARD ONYANGO na VALENTINE OBARA

CHAMA cha ODM kimeonekana kujutia mkataba wa maelewano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama hicho, Raila Odinga.Hii ni kufuatia mzozano wa kisheria ambao unatishia kunyima chama hicho nafasi ya unaibu gavana katika Kaunti ya Nairobi.

Baada ya madiwani wa ODM kuongoza wenzao katika kumng’oa mamlakani aliyekuwa gavana Mike Sonko, chama hicho kilitarajia kupewa nafasi ya naibu wa gavana.

Hata hivyo, wataalamu wa kisheria na duru katika Chama cha Jubilee wanasema huenda ODM isipate nafasi hiyo kwa vile hakuna mkataba rasmi wa ushirikiano kati ya vyama hivyo viwili.

Makubaliano ya handsheki yalihusu tu masuala ya kitaifa yanayofaa kurekebishwa, ilhali mikataba ya ushirikiano wa kisiasa huhitajika kuwasilishwa kwa afisi ya msajili wa vyama.Ijapokuwa Bw Odinga husisitiza kuwa ushirikiano wake na Rais hautatikisika, jana ishara zilionyesha hali si shwari.

Kamati Kuu ya kitaifa ya chama hicho ilikutana Nairobi na katika kikao cha wanahabari, Katibu Mkuu Edwin Sifuna akatangaza kuwa kuendelea mbele chama hicho kitajihadhari kuhusu makubaliano yake na vyama vingine.

‘Ili kulinda na kujenga maslahi ya chama kote nchini, kuanzia sasa kamati hii itasisitiza kuwe na makubaliano rasmi na vyama vingine kuhusu masuala ya aina yoyote,’ akasema Bw Sifuna.

Alisema ODM itasisitiza kuteua mwanachama awe naibu gavana, punde baada ya mahakama kuruhusu mchakato wa kumwapisha gavana mtarajiwa Anne Kananu kuendelea mbele.Katika siku za hivi majuzi, baadhi ya viongozi akiwemo Seneta wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Makadara George Aladwa, wamekuwa wakieleza hofu kwamba huenda Jubilee ikamchezea shere Bw Odinga.

Wakati huo huo, chama hicho kimeanza mchakato wa kutafuta mwaniaji wa urais atakayepeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa 2022.

Bodi ya Uchaguzi ya ODM (NEB) inatarajiwa kuchapisha tangazo magazetini wiki hii la kuwataka Wakenya wanaotaka kuwania urais kupitia chama hicho kutuma maombi.

Viongozi wa ODM ambao tayari wametangaza azma yao ya kutaka kuwania urais ni magavana Wycliffe Oparanya (Kakamega), Hassan Joho (Mombasa) na Amason Jeffah Kingi (Kilifi) pamoja na Bw Odinga ambaye aliwania urais kwenye chaguzi za 1997, 2017, 2013 na 2017.

Japo ameonyesha dalili kuwa huenda akawania urais 2022, Bw Odinga hajatangaza wazi kuwa atajitosa kwenye kinyang’anyiro. Tayari Bw Joho na Bw Kingi wametishia kuunda chama kipya kitakachotetea masilahi ya watu wa Pwani.Iwapo viongozi wawili hao wa Pwani watajiondoa, basi Bw Oparanya huenda akakabidhiwa tiketi ya ODM endapo Bw Odinga hatatuma maombi ya kutaka kuwania urais kwa mara ya tano.

Tangu chama cha ODM kubuniwa mara baada ya Wakenya kutupilia mbali kura ya maamuzi ya kutaka kubadilisha katiba mnamo 2005, hakuna mwanasiasa mwingine tofauti na Bw Odinga ambaye amewahi kuwania urais kupitia tiketi ya chama hicho.Bw Odinga alitumia tiketi ya ODM kuwania urais bila mafanikio katika uchaguzi wa 2007, 2013 na 2017.

You can share this post!

Vyama vipya vinaundwa kwa misingi ya ukabila – Msajili

Wanafunzi 170,000 waliokosa kurejea shuleni wasakwa