• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
KING’ORI: Visa vya wanafunzi kushambulia walimu lazima vidhibitiwe

KING’ORI: Visa vya wanafunzi kushambulia walimu lazima vidhibitiwe

NA KINYUA BIN KING’ORI

WANAFUNZI wamerejea shuleni juzi tu baada ya kukaa nyumbani kwa takriban miezi tisa kutokana na janga la corona.

Lakini katika siku za hivi punde baada ya kurejea kwao, kumekuwa na matukio ya kushangaza kutoka kwa baadhi yao.Ni suala la kusikitisha kuona kuwa mwanafunzi anaamua kubeba silaha na kuamua kumshambulia mwalimu wake.

Majuzi, mwanafunzi wa kidato cha tatu wa shule ya upili ya Kisii High alisababisha shughuli za masomo kukatizwa kwa muda alipomjeruhi mwalimu wake kwa madai ya kumwadhibu huku pia akimjeruhi mwingine aliyeenda kumsaidia mwenzake.

Pia kumekuwa na kisa cha mwanafunzi kupatikana akiwa na panga shuleni katika Kaunti ya Kwale, miongoni mwa vingine. Vitendo hivyo, japo huenda tukaviona vichache leo ni thibitisho kwamba wanafunzi huenda ikawa wamerithi tabia potovu kutoka kwa jamii au wazazi kwa muda wa miezi tisa ambayo wamekaa nje kutokana na ugonjwa wa corona.

Kibarua kigumu tulichonacho kwa sasa ni vipi tunaweza kukomesha visa vya aidha hii. Serikali inafaa kurejesha adhabu ya kiboko shuleni au ibuni mbinu mbadala ya kurejesha nidhamu shuleni, ni lazima mazingira ya mwalimu yawe salama shuleni na nje ya shule kama ya mwanafunzi yalivyo.

Usalama wa mwalimu wafaa kuboreshwa ili wasijeruhiwe na wanafunzi waliopotoka kimaadili.Walimu nchini wanataka kutekeleza wajibu wao katika mazingira bora wala si vinginevyo.

Kwa muda mrefu tumeishi kuangazia usalama wa wanafunzi na kusahau walimu. Mfano, wiki jana vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti visa mbalimbali vya walimu kujeruhiwa, Lakini inasikitisha kuona licha ya matukio hayo ya utovu wa nidhamu kutokea wazazi wamekaa kimya hawajajitokeza hadharani kushtumu visa hivyo.

Hali ingekuwa tofauti ikiwa ni mwalimu angekuwa amemdunga mwanafunzi kisu. Hata hivyo, hali hii inafaa kudhibitiwa kwani ikiwa wanafunzi wataendelea na vitendo vya kushambulia walimu wao, bila shaka viwango vya vlimu vitashuka mno, maana walimu watakuwa wakifanya kazi zao kwa uoga.

Wizara ya Elimu haipaswi sasa kunyamaza walimu wakishambuliwa, hatutaki mwalimu auliwe shuleni na wanafunzi ndio tuanze kukaa vikao kutafuta suluhu. Waziri wa Elimu, Prof George Magoha ahakikishe kuwa serikali inawalinda walimu dhidi ya visa vya aina hii.

Na ili elimu iweze kusaidia kufanikisha nchi na vizazi vijavyo, lazima wanafunzi waweze kuwa wenye nidhamu shuleni hata wakiwa katika mazingira tofauti.

You can share this post!

Toyota Kenya kutuza mwanafunzi bora Sh500,000 katika...

Aina mpya ya corona kutoka Afrika Kusini yafika Kenya