• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
Pigo kwa Jumwa na Tangatanga wakizimwa Kadu

Pigo kwa Jumwa na Tangatanga wakizimwa Kadu

Na CHARLES LWANGA

WANASIASA wa pwani wanaomuunga mkono Naibu Rais William Ruto wamepata pigo kuu, baada ya juhudi zao za kuzindua upya chama cha Kadu Asili kugonga mwamba.

Kiongozi wa Kadu Asili, Bw Gerald Thoya, amemtaka msajili wa vyama vya kisiasa kuingilia kati akidai chama chake “kimeingiliwa kinyume cha sheria” na watu anaoamini wanataka “kusababisha mgogoro wa kisiasa na kiusimamizi katika chama.”

Wabunge Aisha Jumwa (Malindi) na Owen Baya (Kilifi Kaskazini), walioasi ODM, ndio wataathirika zaidi kwani walikuwa mstari wa mbele kupigia debe uzinduzi upya wa Kadu Asili kama chama cha kisiasa cha Pwani.

Uzinduzi huo ulitazamiwa kufanyika mwezi Machi baada yao kukibadilisha jina ili wakitumie kama chombo chao katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Viongozi wengine wa Pwani wanaoegemea mrengo wa Tangatanga, unaohusishwa na Dkt Ruto, ni pamoja na Mohamed Ali (Nyali), Khatib Mwashetani (Lungalunga), Sharif Ali (Lamu Mashariki), Jones Mlolwe (Voi), Paul Katana (Kaloleni), Ali Wario (Bura), Benjamin Tayari (Kinango) na aliyekuwa Seneta wa Mombasa Hassan Omar.

Akizungumza na Taifa Leo mnamo Alhamisi, kiongozi wa Kadu Asili, Bw Thoya, alisema kuwa alistaajabishwa na hatua ya “wanasiasa fulani wa Pwani” kujitosa chamani bila uongozi kufahamishwa, kiasi cha kubadilisha katiba ya chama ili kukidhi maslahi yao.

“Nilimwandikia barua Msajili wa Vyama vya Kisiasa baada ya kujua kuwa baadhi ya watu walikuwa wamevamia chama chetu, kiasi cha kubadilisha katiba, ishara, rangi na kauli mbiu pasipo uongozi kufahamishwa.

“Hatutakubali hilo kwa sababu Kadu Asili ni chama cha kitaifa kinachojisimamia vyema, chenye uongozi thabiti unaoendeshwa kwa mujibu wa Sheria za Vyama vya Kisiasa na Katiba ya Kenya,” alisisitiza Bw Thoya.

Kadu Asili ni miongoni mwa vyama vya kisiasa vinavyosubiriwa kwa hamu mno kutumiwa na wanasiasa katika uchaguzi wa 2022.

Baadhi ya wanasiasa wa mrengo wa Tangatanga eneo la Pwani walidhamiria kukibadilisha jina na kukifanya maarufu eneo hilo ili kukitumia kugombea nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye kura ijayo.

Bi Jumwa ametangaza nia yake ya kutema chama cha ODM, kinachoongozwa na kinara Raila Odinga, na kugombea kiti cha ugavana cha Kilifi 2022 kwa tiketi ya Kadu Asili; huku akiunga mkono azma ya urais ya Dkt Ruto ya 2022.

Alikuwa ameanza kupigia debe vilivyo chama cha Kadu ili kuvutia wanachama wapya na kupata ufadhili kutoka kwa Dkt Ruto.

Wiki mbili ilizopita, mbunge huyo wa Malindi alianzisha kampeni kali kupeperusha Kadu Asili na kusajili wanachama wapya, katika mkutano ulioandaliwa nyumbani kwake Kakuyuni, Malindi.

Hata hivyo, mwenzake wa Kilifi Kaskazini, Bw Baya, alisusia mkutano huo licha ya kuwa miongoni mwa wageni wa heshima walioalikwa kuhudhuria.

You can share this post!

ODM pia ilaumiwe kwa uzembe wa serikali – Ruto

Uingereza yapendekza wanaougua corona walipwe Sh65,000