• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Olunga aahidi kuvumisha Al Duhail katika mahojiano yake ya kwanza

Olunga aahidi kuvumisha Al Duhail katika mahojiano yake ya kwanza

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA Michael ‘Engineer’ Olunga ameahidi makubwa katika mazungumzo yake ya kwanza tangu ajiunge na mabingwa wa Ligi Kuu ya Qatar (QSL) Al Duhail mnamo Januari 12, 2021 akitokea Kashiwa Reysol inayoshiriki Ligi Kuu ya Japan.

Katika kikao na wanahabari kabla ya mechi yake ya tatu, Olunga alitanguliza kuwa anafurahia familia yake mpya ya wachezaji.

Kisha, aliahidi kusaidia Al Duhail kubwaga Al Ahli Doha katika mechi ya raundi ya 16-bora ya Amir Cup itakayosakatwa leo Jumatatu pamoja na mashindano mengine yote.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 26 alisema kuwa kila mtu kambini mwa Al Duhail yuko tayari kwa mtihani wa Al Ahli.

“Tunasubiri mechi hiyo muhimu ambayo pia ni ngumu, lakini tuko tayari na kila mtu anajitahidi kufanya vyema ili tuingie raundi ijayo ya mashindano hayo.”

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Kenya aliongeza, “Niko tayari kwa majukumu nitakayopewa na kocha na nitakuwepo kusaidia timu yangu katika mashindano yote nitakayohitajika pamoja na mechi nyingine yoyote ili tupate ushindi.”

Olunga, ambaye aliibuka Mchezaji Bora wa Mwaka 2020 na pia Mfungaji Bora kwenye Ligi Kuu ya Japan mwaka 2020, alihitimisha kwa kusema anafurahia makao yake mapya.

“Nimechezea timu yangu mpya michuano miwili na unaofuata utakuwa wa tatu. Soka haina tofauti unaisakata Doha, Japan ama nchi nyingine yoyote. Kitu muhimu ni mchezaji kuwa mwepesi wa kukubali mabadiliko kufuatana na mazingira na ninafurahia kuwa na wachezaji wenza wapya.”

Mechi ya Amir Cup kati ya Al Duhail na Al Ahli itapigiwa ugani Grand Hamad. Al Duhail, ambao ni wenyeji, wamekanyaga Al Ahli mara tisa mfululizo kwa jumla ya mabao 31-7 kwa hivyo bado wanapigiwa upatu kuendeleza ukatili wao huo.

Katika klabu yake mpya, Olunga atakuwa na majukumu zaidi kuliko Kashiwa. Tofauti na Kashiwa ambako majukumu yalikuwa ya nyumbani tu, Al Duhail inashiriki Klabu Bingwa bara Asia na pia ni mwenyeji wa Klabu Bingwa Duniani mnamo Februari 4-1.

Al Duhail itafungua kampeni yake ya Klabu Bingwa Duniani dhidi ya miamba wa Afrika Al Ahly katika mechi ya raundi ya pili mnamo Februari 4. Mshindi kati ya Al Duhail ya kocha Sabri Lamouchi na wafalme hao wa Misri atatinga nusu-fainali kupepetana na mabingwa Klabu Bingwa Ulaya Bayern Munich kutoka Ujerumani.

Mechi nyingine ya raundi ya pili itakutanisha mabingwa Amerika ya Kati, Kaskazini na Caribbean (CONCACAF) Tigres UANL kutoka Mexico na wale wa Bara Asia Ulsan Hyundai kutoka Korea Kusini. Mshindi hapa atamenyana katika nusu-fainali na mshindi wa Amerika ya Kusini (CONMEBOL) ambaye atajulikana Januari 30 wakati klabu za Brazil Palmerais na Santos zitakabana koo katika fainali ya Libertadores. Makala ya 2020 ya Klabu Bingwa Duniani, ambayo yaliahirishwa kutoka Desemba mwaka jana kutokana na mkurupuko wa virusi vya corona, atafahamika hapo Februari 11.

You can share this post!

BI TAIFA JANUARI 25, 2021

Watamjaribu Baba?