• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:23 PM
WARUI: Hatua ya dharura yahitajika kuzima utovu wa nidhamu shuleni

WARUI: Hatua ya dharura yahitajika kuzima utovu wa nidhamu shuleni

Na WANTO WARUI

TANGU kufunguliwa kwa shule mwezi huu wa Januari, visa kadha wa kadha vya utovu wa nidhamu vimetokea shuleni vikisababishwa na wanafunzi.

Kuna tetesi katika shule nyingi kuwa wanafunzi wamepoteza mwelekeo na hali yao ya nidhamu ni mbaya.

Kisa kilichotokea kule Kisii cha mwanafunzi wa kidato cha tatu kuwadunga visu walimu wake wawili ni cha kuatua moyo. Mwanafunzi huyu ambaye alikuwa amechelewa kufika gwarideni aliulizwa na mwalimu sababu ya kuchelewa. Alipoambiwa apige magoti, alienda kwenye bweni akachukua kisu ambacho alitumia kumdunga mwalimu huyo. Mwalimu wa pili naye alidungwa akijaribu kumsaidia mwenzake.

Juma lililopita, mwanafunzi wa miaka 17 wa shule ya Wavulana ya Wahundura, Mathioya katika kaunti ya Murang’a alifikishwa katika hospitali kuu ya Kenyatta kupata matibabu ya dharura baada ya kudungwa kisu na mwanafunzi mwenzake. Mwanafunzi huyo, Simon Muchunu, anasemekana kuwa alidungwa kisu kichwani na mwenzake wa kidato cha tatu baada ya kugombana kuhusu kufuli.

Kwingineko, mwanafunzi wa Gredi ya 4 katika shule ya msingi ya Kegati, Nyaribari Chache, Kaunti ya Kisii alijaribu kumuua baba yake kwa kumtilia sumu kwenye uji. Baba yake mwanafunzi huyo alikuwa amemwuliza kuhusu uhusiano wake wa kimapenzi na mwanafunzi mwingine wa Kidato cha Nne ambapo mtoto huyo alikasirika.

Visa hivi na vingine vingi ambavyo vinajitokeza, vinatuchorea taswira ya jinsi ambavyo utovu wa nidhamu umeshamiri miongoni mwa wanafunzi. Pana haja ya washika dau wa elimu ikiwemo Wizara ya Elimu, wazazi na walimu kuharakisha kutafuta mbinu mwafaka za kukabiliana na hali hii kabla mambo hayatumbukia nyongo.

Kipindi kirefu ambapo wanafunzi wamekaa nyumbani kutokana na athari ya mkurupuko wa gonjwa la Covid-19, kimesababisha hasara kubwa sana kwa wanafunzi. Wazazi wengi walishindwa kuwadhibiti watoto wao na kuwaacha wafanye watakavyo.

Wasichana wengi walijiingiza katika mapenzi ambayo yaliishia kwa mimba na maradhi ya zinaa. Wavulana nao waliingilia tabia za kihuni kama matumizi ya dawa za kulevya, wizi na ukora mwingine.

Ilivyo sasa shuleni, walimu wanakabiliwa na hali ngumu ya kudhibiti nidhamu. Wanafunzi walio shuleni sasa sio wale waliokuwamo miezi tisa iliyopita. Wamebadilika kabisa. Wengi wao wamepotoshwa, asilimia kubwa ikikosa maadili.

Pia ni muhimu walimu wawe macho sana ili kuzuia vifaa visivyotakikana shuleni kama vile visu kuingizwa ndani ya maeneo ya kusomea.

Wazazi, ambao inathibitika sasa kuwa wametelekeza wajibu wao wa malezi hawana budi kuinuka na kufanya jinsi wanavyotakiwa kufanya.

Mambo haya yote ambayo yanatokea yanaonyesha kuwa kunahitajika njia mpya na za haraka za kukabiliana na utovu wa nidhamu shuleni ikiwemo mashauriano miongoni mwa nyingine.

You can share this post!

ONYANGO: Ushauri nasaha ndio dawa ya matatizo ya akili,...

DIMBA: ‘Big Mo’ Kean ametajwa kama kizazi kipya...