• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
UDAKU: Neymar hapoi! Sasa amejinasia kidege Emilia wa Argentina

UDAKU: Neymar hapoi! Sasa amejinasia kidege Emilia wa Argentina

Na CHRIS ADUNGO

NYOTA wa Paris Saint-Germain (PSG), Neymar Jr, 28, amepata hifadhi mpya ya penzi lake kwa mwanamuziki maarufu raia wa Argentina, Emilia Mernes.

Kwa mujibu wa gazeti la The Sun, wawili hao walianza kubadilishana arafa za kimahaba baada ya Emilia kuhudhuria hafla ya kufunga mwaka 2020, iliyoandaliwa na Neymar jijini Rio de Janeiro, Brazil.

Dhifa hiyo ya siku tatu iliyopagazwa jina ‘Neymarpalooza’, ilihudhuriwa na watu 500 wakiwemo wanamitindo Kiki Passo, Michelle Nevius na Jessica Bartlett kutoka Amerika. Vile vile, makahaba Camila Remedy na Fernanda Brum kutoka Brazil walikuwepo.

Siku ya mwisho Neymar alionekana akisakata densi na Emilia, 24, huku wakiimba kwa pamoja kibao cha hivi punde cha mwanamuziki huyo: “Siendi tena msituni kuwinda wakati kuna mbalamwezi. Waambie vipusa wanaokufuata kwamba mimi ni chaguo lako.”

Akihojiwa na The Sun wiki jana, Lizardo Ponce, ambaye ni rafiki wa karibu wa Emilia, alikiri kwamba Neymar alimtembelea kidege huyo nchini Argentina majuma mawili yaliyopita.

“Emilia amekuwa akimsifia sana Neymar; jinsi alimridhisha chumbani, alivyo mkarimu na pia mcheshi. Ilivyo, kilele cha urafiki wao ni ndoa. Tuwape muda; yaliyopo kati yao yatajitokeza,” akaeleza Lizardo na kuongeza kwamba dalili zote zinaashiria wawili hao wanakula bata, na haitakuwa ajabu wakivishana pete za uchumba karibuni.

Baada ya mahojiano hayo, Neymar alipakia kwenye Instagram picha yake na Emilia.

Naye kidosho huyo akajibu kwa picha nyingine akitia ‘emoji’ za furaha na kuandika: “Nakupenda kwa moyo wangu wote, na mimi huamini katika miujiza ya mwanzo bora kwa kila jambo jipya.”

Tangu Neymar atemane na mwigizaji raia wa Brazil, Bruna Marquezine, sogora huyo wa zamani wa Barcelona ametoka kimapenzi na vidosho wa kila sampuli, akiwemo mwanamitindo raia wa Amerika, Natalia Barulich.

Hata hivyo, walitengana mwanzoni mwa Desemba 2020 baada ya nahodha huyo wa timu ya taifa ya Brazil kuanza kumtambalia kimapenzi mwanamitindo na mwanahabari wa Uhispania, Melodie Penalver.

Awali, gazeti la Proto Thema nchini Ugiriki lilisema kwamba Neymar alikuwa radhi kuliwania upya tunda la Bruna baada ya Melodie kuanza kumfungulia mzinga mwigizaji Cristian Jerez aliyewahi kushirikiana naye kuendesha kipindi cha ‘Temptation Island’ kwenye mojawapo ya runinga za Uhispania.

Neymar amekuwa singo tangu atengane rasmi na Bruna aliyemburudisha kimapenzi kwa miaka sita. Hadi kufichuka kwa uhusiano wake na Emilia, Neymar aliwahi pia kuchovya kwenye mizinga ya warembo Liza Brito, Danna Paola, Mari Tavares, Larissa de Macedo Machado almaarufu Anitta na Ellen Santana aliyetawazwa mshindi wa Miss BumBum nchini Brazil mnamo 2018.

Penzi la Neymar limewahi pia kuwaniwa na vipusa Giovanna Lancelotti, Sabine Jemeljanova, Selena Gomez, Soraja Vucelic, Chloe Grace Moretz, Noa Saez, Izabel Goulart na Alsessandra Ambrosio.

Neymar ana mtoto mmoja wa kiume – Davi Lucca da Silva Santos aliyezaliwa na mrembo raia wa Brazil Carolina Dantas, 27, mnamo Agosti 24, 2011.

Mmoja wa mashabiki wa Emilia kwenye Instagram aliandika: “Nashawishika kuiamini safari hii ya mapenzi. Tamanio langu sasa ni kuona Neymar na Emilia wakila yamini ya ndoa.”

You can share this post!

Man-United wadengua Liverpool katika Kombe la FA na kufuzu...

Chelsea wamtimua kocha Frank Lampard baada ya miezi 18