• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
TAHARIRI: Mzozo mpakani na Somalia utatuliwe

TAHARIRI: Mzozo mpakani na Somalia utatuliwe

KITENGO CHA UHARIRI

USALAMA wa nchi ni moja kati ya mambo makuu ya utawala wowote ulimwenguni.

Kenya kwa upande wetu, tunailinda nchi usiku na mchana kupitia vikozi mbalimbali vya jeshi la nchi (KDF).

Hata tunapokuwa tumelala, vijana wetu wa jeshi la angani, jeshi la majini na lile la nchi kavu, hukaa imara kuhakikisha kwamba hakuna adui yeyote anayeweza kutuvamia.

Kutokana na kujitolea kwa wanajeshi wetu na kiwango chao cha juu cha nidhamu, wamewahi kualikwa katika harakati nyingi za kurejesha amani katika mataifa kama Kosovo, Sierra Leone na katika eneo la Darfur, Sudan kati ya mengine.

Usalama wa nchi yetu ni muhimu zaidi, na haifai kuuhatarisha kwa kuruhusu mahasimu kutoka taifa jirani waendeleza uhasama wao katika ardhi yetu. Mapigano yanayoendelea kati ya Jeshi la Somalia na lile la Jubaland karibu na mji wa Mandera, yanaiingiza nchi katika hatari ya kugeuzwa uwanja wa mapigano.

Wanajeshi wa Somalia chini ya utawala wa Rais Mohammed Abdullahi Farmaajo na wale wa Jubbaland walio watiifu kwa Rais Ahmed Madobe, walikabiliana katika mji wa Bulahawa karibu na Mandera na kuvuruga shughuli mchana kutwa.

Inasemekana kuwa wanajeshi wa Somalia wanamsaka waziri wa Usalama wa Jubbaland, Abdirashid Hassan Abdinur maarufu kama Abdirashid Janan ambaye amekuwa mafichoni mjini Mandera.

Tangu wakati huo, Bw Janan amekuwa akijipanga ili kuteka mji huo wa Bulahawa.

Inasemekana amekuwa akipokea silaha kutoka Kismayu na kuimarisha kikosi chake cha jeshi kabla ya mashambulizi ya Jumatatu.

Kwa siku yote, biashara nyingi zilisalia kufungwa mjini Mandera kutokana na makabiliano kati ya wanajeshi hao huku akina mama na watoto wakitorokea usalama wao kwenye mji wa Sufti, ambao upo mpakani mwa Kenya na Ethiopia.

Mnamo Novemba 2020 Rais Farmaajo alimshutumu Rais Uhuru Kenyatta kwa kuandaa mkutano na Rais Madobe, akishikila kwamba Kenya ilikuwa ikimsaidia kiongozi huyo kijeshi ili kuvuruga amani na utawala wake nchini Somalia.

Ingawa Kenya haikujibu madai hayo, suala hili si la kufumbiwa macho. Umoja wa Afrika (AU) wapaswa kuchukua hatua za haraka kuingilia mgogoro huo, unaoweza kuharibu sifa ya Kenya kama kisiwa cha amani.

You can share this post!

WANGARI: KNUT ishirikiane na serikali kuboresha maslahi ya...

Hellen Obiri alenga kuonyesha wapinzani kivumbi kwenye Mbio...