• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Serikali yaweka kafyu, operesheni Kapedo

Serikali yaweka kafyu, operesheni Kapedo

Na CECIL ODONGO

HUKU hali ya usalama ikiendelea kudorora katika eneo la Kapedo kwenye mpaka wa Kaunti za Turkana na Baringo, Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i amesema serikali inalichukulia eneo hilo kama la vita na itaweka kafyu ya mapema.

Kwa sasa nchi nzima ina kafyu ya kuanzia saa nne usiku hadi saa 10 alfajiri. Hata hivyo, kafyu ya Kapedo itaanza saa 12 jioni hadi saa 12 asubuhi.

Zaidi ya watu 10 wamefariki kutokana na uvamizi wa majangili katika eneo la Kapedo kwa muda wa mwezi moja pekee na Waziri Matiang’i pia alifichua kuwa ataweka notisi kwenye gazeti la serikali ili operesheni ya kijeshi iendeshwe eneo hilo.

“Tunataka kumalizana na huu utovu wa usalama kabisa ili eneo hilo lisalie salama. Kutimiza hilo lazima tukabiliane na majangili na viongozi wa kisiasa ambao wanahusika na ukosefu huo wa usalama,” akasema Dkt Matiang’i mnamo Jumatatu baada ya mkutano na Waziri wa Ulinzi wa Uingereza Ben Wallace aliye ziarani hapa nchini.

Hii itakuwa mara ya pili ambapo Kapedo itachapishwa kwenye gazeti la serikali kama eneo hatari zaidi kiusalama baada ya Baraza Kuu la Usalama kufanya hivyo mnamo 2017. Operesheni inayopangwa italenga Rumuruti, Ol Moran, Kirimon, Marmanet, Mukogodo Mashariki, Segera, Mithiga na Matuiku.

Mnamo Alhamisi wiki jana, polisi wawili waliokuwa wakishika doria Kapedo waliuawa kutokana na mashambulizi ya kushtukiza yaliyotekelezwa na majangili hao. Afisa huyo wa cheo cha Inspekta na dereva wake walikuwa kwenye msafara wa magari matatu, waliposhambuliwa katika daraja linalopatikana kwenye mpaka wa kaunti za Turkana na Baringo.

Siku iliyotangulia, miili ya raia sita ilipatikana ikiwa na majeraha ya risasi ikikisiwa waliuawa na majangili hao ambao pia wamekuwa wakiiba mifugo.

You can share this post!

Tyler Onyango afurahia kuchezeshwa na Ancelotti

NAOMI MABEYA: Mama Kayai amekuwa chocheo kwa uigizaji wangu