• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
NAOMI MABEYA: Mama Kayai amekuwa chocheo kwa uigizaji wangu

NAOMI MABEYA: Mama Kayai amekuwa chocheo kwa uigizaji wangu

Na JOHN KIMWERE

ANAAMINI anatosha mboga kufanya vizuri katika tasnia ya maigizo na kitinga upeo wa kimataifa miaka ijayo. Anadai kuwa amepania kujituma mithili ya mchwa ili kutimiza ndoto yake wala hatokubali chochote kuzima ndoto yake.

Naomi Mabera Mabeya maarufu kama Kemunto aliye kati ya waigizaji wanaokuja hapa nchini ni mwanafunzi wa mwaka wa nne kwenye Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU).

Anasema alianza kujituma katika masuala ya uigizaji mwaka 2017 ambapo anadhamiria kuibuka miongoni mwa waigizaji mahiri duniani kama Taraji Penda Henson aliye kati ya walioigiza kwenye kipindi cha Empire. Kando na uigizaji Kemunto anamiliki brandi yake katika mtandao wa Youtube kwa jina ‘Gusii nation TV’ aliyoanzisha mwaka 2019.

VITIMBI

“Ingawa nikiwa mtoto nilitamani sana kuhitimu kuwa wakili kama taaluma yangu maishani bado nilikuwa nashiriki uigizaji tangia nikisoma Shule ya Msingi,” binti huyo alisema na kuongeza kuwa anatamani sana kuibuka staa na kushiriki filamu za hadhi ya Hollywood na Nollywood. Katika mpango mzima anasema alivutiwa na maigizo baada ya kutazama uigizaji wake, Mama Kayai aliyekuwa akishiriki kipindi cha ‘Vitimbi’ kilichokuwa kinapeperushwa kupitia runinga ya KBC.

Anasema ndani ya miaka mitatu iliyopita amebahatika kushiriki filamu nyingi tu ambazo zimepata mpenyo kupeperushwa kupitia runinga kadhaa nchini ikiwamo moja ya mtandaoni iitwayo Ndizi TV. Kati ya filamu hizo zikiwa ‘Selina,’ ‘Njoro wa uba,’ na ‘Nganya,’ (Maisha Magic East), ‘Auntie Boss (NTV) kati ya zingine. Anatoa wito kwa serikali za kaunti zote 47 zifungue vituo vya kukuza talanta za wasanii wanaokuja nchini wavulana kwa wasichana maana wamefurika wengu tu katika kila pembe mwa Kenya.

Naomi Mabera Mabeya maarufu kama Kemunto. PICHA/ JOHN KIMWERE

TOTO DIKEH

Kisura huyu anasema barani Afrika angependa kufanya kazi na waigizaji wengi tu huku akitaja baadhi yao kama: Toto Dikeh na Mercy Johnson ambao wote huigiza filamu za Kinigeria (Nollywood). Kwa wenzie wa humu nchini angependa sana kushirikiana na mcheshi anayekuja Eunice Wanjiru Njoki (Mammito) pia mwigizaji Beatrice Dorea Chege (Maggie Maria).

”Bila kupepesa macho huku na kule nashukuru wafuasi wangu kwa sapoti yao kwa kazi zangu,” alisema na kuongeza kuwa kama haingekuwa wao angefikia kiwango alicho kwa sasa katika masuala ya maigizo.

CHANGAMOTO

Anasema kuwa katika sekta ya maigizo wanapitia changa moto nyingi tu ikiwamo kukosa fedha za kugharamia shughuli zao kikazi.

”Ningependa kushauri wanawake wenzangu kuwa ni muhimu tuwe wabunifu ili kujihepusha dhidi ya changamoto za kukosa ajira. Kiukweli taifa hili lina waigizaji wengi ambapo lakini nafasi sio nyingi,” akasema.

You can share this post!

Serikali yaweka kafyu, operesheni Kapedo

Chipukizi apania kufikia upeo wa Burna Boy