• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Hellen Obiri alenga kuonyesha wapinzani kivumbi kwenye Mbio za Nyika za Majeshi

Hellen Obiri alenga kuonyesha wapinzani kivumbi kwenye Mbio za Nyika za Majeshi

Na AYUMBA AYODI

MALKIA wa Mbio za Nyika Duniani Hellen Obiri analenga kuonyesha wenzake kivumbi kwenye Mbio za Nyika za Majeshi (KDF) katika uwanja wa Moi Air Base jijini Nairobi hapo Ijumaa.

Bingwa huyo wa Riadha za Dunia mbio za mita 5,000 alipoteza taji la KDF mwaka 2020. Anatumai kurejesha taji hilo na kulitwaa kwa mara ya tano pia akilenga kuhifadhi ubingwa wa taifa.

Obiri alishinda taji la KDF kwa mara ya kwanza mwaka 2014 kabla ya kufagia mataji ya mwaka 2017 hadi 2019 akitwaa umalkia wa mbio hizo kitaifa pia miaka hiyo.

Aliingia katika mabuku ya kihistoria kwa kuwa mwanariadha wa kwanza kushinda mataji ya dunia ya Mbio za Ukumbini (mita 3,000), Riadha za Dunia (mita 5,000) na Mbio za Nyika (kilomita 10).

“Natamani kushinda mataji ya KDF na kitaifa tena kabla nizamie msimu wa riadha za uwanjani,” alisema Obiri, ambaye alifungua msimu kwa kutwaa taji la Mbio za Nyika mjini Machakos mnamo Novemba 28.

“Sina cha kunitia hofu wakati huu ninapojitahidi kuwa katika hali nzuri,” alisema Obiri, ambaye ataamua kushiriki mbio za mita 10,000 na mita 5,000 ama moja ya vitengo hivyo kwenye Olimpiki mjini Tokyo baadaye mwaka 2021 baada ya duru mbili za kwanza za Riadha za Diamond League mjini Rabat, Morocco (Mei 23) na Doha, Qatar (Mei 28).

“Ndoto yangu kuu ni kushinda taji la Olimpiki mwaka huu,” alisema Obiri, ambaye aliridhika na medali ya fedha ya mbio za mita 5,000 kwenye Olimpiki 2016 nchini Brazil.

Imetafsiriwa na Geoffrey Anene

You can share this post!

TAHARIRI: Mzozo mpakani na Somalia utatuliwe

NMS kuzindua mpango wa kusafisha jiji la Nairobi na viunga...