• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:55 AM
Kanisa la Glory OutReach Assembly lazingatia kuhubiri amani

Kanisa la Glory OutReach Assembly lazingatia kuhubiri amani

Na LAWRENCE ONGARO

KANISA la Glory OutReach Assembly lililoko Kahawa Wendani limejitolea kuendeleza na kudumisha amani kote nchini kwa kuleta jamii zote pamoja.

Mchungaji wa kanisa hilo Bi Joyce Njeri alisema kanisa hilo kwa siku za hivi karibuni limezuru maeneo yaliyokosa amani ili kuhubiri amani na kuwapa wakazi chakula cha kiroho.

Baadhi ya maeneo ambayo wamezuru ili kuhubiri amani ni Turkana, Pokot na maeneo kavu yanayohitaji mahubiri thabiti.

Bi Njeri ambaye ni mtaalam wa kisaikolojia huku pia akihubiri alisema kipindi hiki cha corona walimekuwa na shughuli nyingi za kuhubiria watu na kuwapa matumaini.

“Tulipata ya kwamba kwa muda huo mrefu ambapo janga la corona lilivamia taifa, familia nyingi zilisambaratika na hata migogoro ilizidi nyumbani. Mimi kama mtaalam wa kiakili nimefaulu kuwapa matumaini makubwa watu wa familia nyingi,” alisema Bi Njeri.

Alisema licha ya waumini wengi kufika makanisani, kuna haja zaidi ya kuwapa ushauri wa jinsi ya kukabiliana na hali ya kimaisha.

Mwishoni mwa wiki kanisa hilo liliadhimisha miaka 30 kwa kuhubiri amani katika jamii huku wakitaka pia madhehebu mengine yawe na mwelekeo huo kote nchini.

Alisema wakati huu taifa linapokaribia uchaguzi mkuu 2022 wachungaji wana jukumu la kuhubiri amani katika maeneo ya ibada kote nchini.

“Iwapo Wakenya kwa jumla watazingatia amani bila kusukumwa na mawimbi ya siasa, bila shaka ifikapo mwaka wa 2022 watakuwa na uchaguzi wa amani usio na chuki na uhasama wa kikabila,” alisema Bi Njeri.

Muumini mmoja wa kanisa hilo Sebazungu Theophile aliye raia wa Rwanda alitoa mwito kwa Wakenya wawe makini na wazingatie amani zaidi.

“Mimi baada ya machafuko ya Rwanda mwaka wa 1994 nilipata shida kubwa wakati wazazi wangu wote waliuawa kinyama mbele yangu. Ilibidi nipate usaidizi kupitia shirika moja lisilo la kiserikali,” alifafanua Theophile.

Naye Bw Mwai Muchiri mkazi wa Githurai 45, ambaye ni mshiriki katika kanisa hilo alisema baada ya kupata ushauri kupitia mchungaji Njeri amerejea maisha yake ya kawaida baada ya kukumbwa na masaibu ya kimaisha chungu nzima.

You can share this post!

NMS kuzindua mpango wa kusafisha jiji la Nairobi na viunga...

Kiungo Mkenya-Mwingereza Henry Ochieng’ atangaza...