Na MASHIRIKA
BEKI Fikayo Tomori wa Chelsea amejiunga na kikosi cha AC Milan kinachoshiriki Ligi Kuu ya Italia (Serie A) kwa mkopo.
Difenda huyo mwenye umri wa miaka 23 aliwajibishwa na timu ya taifa ya Uingereza kwa mara ya kwanza mnamo Novemba 2019.
Kwa mujibu wa gazeti la La Gazzetta dello Sport, AC Milan watakuwa radhi kumpa Tomori mkataba wa kudumu mwishoni mwa muhula huu na kujitwalia kabisa huduma zake kwa kima cha Sh3.5 bilioni.
Tomori ambaye alikosekana kwenye mipango ya baadaye ya kocha Frank Lampard uwanjani Stamford Bridge, aliwajibishwa na Chelsea mara nne pekee msimu huu huku akichezeshwa mara moja pekee kwenye Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).
Sogora huyo alitia saini mkataba wa miaka mitano na Chelsea mnamo Disemba 2019 baada ya kuridhisha katika mchuano uliompa jukwaa la kuvalia jezi za Uingereza dhidi ya Kosovo.
Kabla ya Chelsea kumsajili beki mzoefu Thiago Silva kutoka Paris Saint-Germain (PSG) mwanzoni mwa msimu huu, Tomori aliwajibishwa mara kwa mara na kocha Lampard aliyewahi pia kumtia makali kambini mwa Derby County.