• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Mwigizaji chipukizi shindano la urembo wikendi mtaani Kayole 

Mwigizaji chipukizi shindano la urembo wikendi mtaani Kayole 

Na JOHN  KIMWERE 
 
WAHENGA hawakupaka mafuta kwenye mgongo wa chupa, waliposema kuwa penye nia pana njia, maana ndivyo ilivyo tangia zama hizo na ipo hivyo mpaka sasa.
 
Usemi huo umeonyesha mashiko ya haja miongoni mwa jamii. Aidha ni msemo unaozidi kudhihirishwa na wengi ambao wameamua kujituma kisabuni kwa kujiamini wanaweza kusudi watimize malengo yao maishani.
 
MR na MISS
 
Valary Akinyi ni miongoni mwa waigizaji wanaozidi kuvumisha tasnia ya filamu nchini ingawa bado hawajashika mashiko.
Licha ya janga la corona kupiga shopu shughuli nyingi duniani, msanii huyu kupitia brandi yake ‘Nawiri Arts Productions’ aliandaa shindano la vijana kutafuta Miss na Mr Lower Savannah mtaani Kayole, Nairobi.
 
Shindano hilo lililofanyika Desemba livutia wafuasi wengi katika eneo hilo.
 
”Tunalenga kukuza talanta za vijana mitaani huku tukidhamiria kutumia shindano hilo kuwasaidia kujihepusha dhidi ya matendo maovu,” dada huyo alisema na kuongeza kuwa ndani ya kipindi hiki wengi wamejikuta njia panda kwa kukosa ajira.
 
Dada huyu anasema shindano hilo lilijumuisha jumla ya washiriki 20, wasichana kumi sawa na wavulana ambapo washindi tatu wa kwanza katika kila jinsia watatuzwa.
 
Msanii huyu anashukuru wenzake wanaoibuka na wazo hilo linalenga kusaidia vijana wa eneo hilo kutambua talanta zao katika masuala ya urembo.
 
 
Akinyi (27) ameandaa shughuli hizo akishirikiana na wenzako akiwamo Rael ‘Recho’ Ondipo, David Ongano, Elisha Arua na Starford Ochieng.
 
STUCKING IN THE MIDDLE
 
Kando na uigizaji dada huyu ni produsa anajivunia kuzalisha filamu kama:  ‘Mambo mambo’, ‘Stucking in the Middle’, ‘The Orphan’, ‘The Highway,’ na ‘Vundo series’ chini ya kundi liitwalo Bandilisha Arts Production.
 
Kisura huyu anayejivunia kuwa katika tasnia ya uigizaji kwa miaka minane anadokeza kuwa bado analenga kusaidia wenzake wanaokuja kutambua vipaji vyao na kuwasaidia siku sijazo.
 
Katika maigizo  binti huyu anajivunia kushiriki vipindi tofauti ikiwemo Auntie Boss (NTV), Daktari (KTN), Real Househelp of Kawangware (KTN) na  Hulabaluu (Maisha Magic East).
 
Anataka mashirika yanayomiliki vyombo vya habari nchini kuanzisha vipindi zaidi kupeperusha filamu zinazozalishwa na wazalendo ili kuwapa ajira wasanii chipukizi.
 
MCHOYO 
Binti huyu kamwe sio mchoyo anashauri wenzake wanaoibukia kuwa wavumilivu na wafanye kazi kwa kujitolea hata wakipata nafasi gani. Anawaambia kuwa kujituma kwao kutachangia watambulike wanatosha mboga katika maigizo.
 
Pia anashauri wasanii chipukizi kuwa endapo wanahisi wana talanta wasisubirie miaka iende mbali muda ndio huu watafute jinsi ya kuingia katika ulingo wa maigizo.
 
Hata hivyo anashikilia kuwa uigizaji siyo mteremko unahitaji nidhamu, kujitolea na kujituma bila kulegeza kamba vile vile pia kumtegemea Mungu zaidi.

You can share this post!

LISHE NA VINYWAJI: Manufaa ya juisi

Raila aambia Mlima Kenya wamlipe ‘madeni’ yake 2022