• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 11:55 AM
KINA CHA FIKIRA: Ukijiamini kwa lolote utafanikiwa hivyo hivyo ulivyo

KINA CHA FIKIRA: Ukijiamini kwa lolote utafanikiwa hivyo hivyo ulivyo

Na WALLAH BIN WALLAH

MAFANIKIO hupatikana kwa bidii pamoja na jinsi mtu anavyojiamini katika shughuli au kazi anazofanya maishani.

Usidhani mtu hufanikiwa au hufaulu kwa kuwa ameumbwa tofauti ama anavyo viungomwili vya ziada kuliko wewe!

Usidhani mwenzako ana vichwa viwili, mikono mitano, macho sita, masikio manne ama miguu zaidi ya miwili! La hasha! Wengine ni wadogo, wembamba na wafupi zaidi yako! Lakini wanafanya mambo makubwa, matendo bora na kazi njema zaidi kwa kujiamini na kuamini kwamba hakuna kisichowezekana kwa mtu mwenye nia anayejituma!

Kijana mdogo aitwaye Karatasi alipokuwa na umri wa miaka kumi, aliamua kujifunza michezo ya judo na karate. Lakini balaa ilitokea! Kijana Karatasi alipata ajali kwenye gari. Mkono wake wa kushoto ulivunjika kenyekenye!

Alipolazwa hospitalini, madaktari waliamua kuukata. Karatasi akabaki na mkono mmoja tu wa kulia! Ajali ilimkata mkono lakini haikumkatisha tamaa ya kujifunza karate na judo! Baada ya kutoka hospitalini alipopona kabisa, alienda kwa Mwalimu wa judo na karate akamwambia, “Mwalimu, nimekuja unifundishe!” Mwalimu Yaimoto alimtazama na kumchuja kwa macho ya maswali. Akajibu, “Sawa Karatasi! Nitakufundisha! Tuanze lini?”

Karatasi alimwambia Mwalimu, “Ninaomba tuanze kesho ili leo nikanunue sare pamoja na vifaa vinavyohitajika!” Kesho yake Karatasi alienda kuanza kujifunza baada ya kulipia ada! Alianzia mafunzo ya judo. Kwa muda wa miezi mitatu aligundua kuwa Mwalimu alikuwa akimfunza mtindo mmoja tu wa kuutumia mkono wake mmoja wa kulia pamoja na miguu. Alielewa kuutumia na kujikinga vizuri zaidi.

Walipofanya mazoezi na majaribio ya kupigana na Mwalimu wake, Mwalimu alitokwa jasho! Siku moja Karatasi alimuuliza Mwalimu wake, “Mbona unanifunza mtindo mmoja tu wa kupambana na kujihami?” Mwalimu Yaimoto alimjibu, “Heri mtu anayejua mbinu moja anayoamini na kujiamini kwamba anaweza kuitumia vizuri kuliko ajuaye mambo mengi yasiyomsaidia! Muhimu ni kujiamini!”

Baada ya siku kadhaa Karatasi alihitimu kozi za judo na karate. Mwalimu Yaimoto alimpeleka kwenye mashindano makubwa ya kitaifa katika ukumbi Mkuu jijini Kumbuko. Zamu yake ilipofika na akapanda jukwaani, kila mtu alishtuka kumwona kijana mdogo mwenye mkono mmoja akirukaruka jukwaani kusubiri kipenga apambane na Nyundonyundo; jitu la miraba minne kwenye karate!

Refarii alipopuliza kipenga, Karatasi alimrarua mpinzani wake Nyundonyundo kwa kutumia mkono mmoja na mateke! Akamwangusha chini mara nyingi bila kumpa nafasi! Kwenye dakika tano za kwanza, Nyundonyundo alianguka chini tena akashindwa kunyanyuka! Refarii akatangaza, “Mchezo umekwisha!” Karatasi alishinda kwa kishindo!!

Ndugu wapenzi, mtu akijiamini katika kutenda mambo au kazi ama shughuli zake vizuri, atafaulu hivyo hivyo alivyo! Tujiamini!!!!

You can share this post!

Wasiwasi huku vituo vya damu vikikauka

TAHARIRI: Tuhimize maadili kwa watoto wetu