• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:55 PM
Murathe sasa akiri kauli ya Kang’ata ni kweli kuhusu BBI kususiwa

Murathe sasa akiri kauli ya Kang’ata ni kweli kuhusu BBI kususiwa

Na WANDERI KAMAU

NAIBU Mwenyekiti wa Chama cha Jubilee, David Murathe, Alhamisi alimtetea Seneta Irungu Kang’ata wa Murang’a, akisema alieleza ukweli kuhusu hali ilivyo katika Mlima Kenya kuhusu ripoti ya Mpango wa Maridhiano (BBI).

Majuma matatu yaliyopita, Seneta Kang’ata alimwandikia barua Rais Uhuru Kenyatta akimwambia kuchukua hatua za haraka kutatua changamoto zinazowaathiri wenyeji wa Mlima Kenya, kwani wengi wao hawaungi mkono ripoti hiyo.

Licha ya Dkt Kang’ata kukosolewa vikali na baadhi ya wanasiasa wanaomuunga mkono Rais Kenyatta, Bw Murathe alisema kuwa seneta huyo hapaswi kukosolewa kwani alisema ukweli, lakini alitumia njia isiyofaa.

Kwenye barua hiyo ambayo ilizua hisia kali za kisiasa katika ukanda huo, Dkt Kang’ata alionya kuwa huenda juhudi za Rais Kenyatta kuwarai wenyeji kuunga mkono BBI zikakosa kuzaa matunda, ikiwa serikali haitaeleza mikakati ya kuboresha hali ya uchumi na kufufua upya sekta ya kilimo.

Akionekana kukubali kulikuwa na tatizo kuhusu jinsi mikakati ya kuipigia debe ripoti hiyo Mlima Kenya ilikuwa ikiendeshwa, Bw Murathe aliwakosoa viongozi waliotwikwa jukumu hilo kwa kuwalazimishia wananchi kukubali BBI.

“Huwezi kuwalazimishia wenyeji jambo bila kuwaelezea au kuwafafanulia ukweli. Hilo ndilo tatizo kuu lililokuwepo. Hata hivyo, tunalenga kulainisha shughuli za kuipigia debe BBI baada ya mkutano wa viongozi wa eneo hilo utakaofanyika kesho Sagana,” akasema.

Wakati huo huo, Bw Murathe alifichua kwamba Rais Kenyatta ndiye aliyewazuia kuwachukulia hatua za kinidhamu maseneta maalum waasi chamani kama Isaac Mwaura, Millicent Omanga na Mary Seneta.

Alisema usimamizi mkuu wa chama ulikuwa tayari umeanza mchakato wa kuwafukuza chamani lakini Rais akawarai kusitisha.

You can share this post!

Presha kwa Raila akae kando 2022 aachie wengine

Joho amruka Kingi kuhusu kugura ODM