• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
CHOCHEO: Ukikutana na EX itakuwaje?

CHOCHEO: Ukikutana na EX itakuwaje?

Na BENSON MATHEKA

“NIMEFIKA mwisho. Nataka talaka. Siwezi kuvumilia maisha kama haya,” Liza alimweleza Peter.

Hii ilikuwa baada ya wawili hao kugombana vikali Peter akimlaumu kwa kutochangia katika bajeti ya nyumba licha ya kuwa na kazi na mshahara mkubwa.

Lakini pia alimsihi asimtaliki akisema kwamba kuvunja ndoa yao kungeathiri watoto wao wawili. Liza alimkumbusha kwamba ni yeye anayewashughulikia watoto hao na hangekubali awatumie kuendelea kumtesa. “Nimeamua na sibadilishi nia. Umenifanya mtumwa kwa miaka saba sasa,” akasema.

Siku iliyofuata, wakili wa Liza alimpelekea Peter stakabadhi za talaka na akazikubali. Ni miaka miwili sasa na Liza na Peter ni marafiki ingawa walitakiana. “Nafurahia uhuru wangu naye huniambia anafurahia maisha yake mapya. Anawatembelea watoto kwa kuwa ninaishi nao na huwa nawapeleka kwake pia na kumpatia uroda kwa kuwa nafurahia ustadi wake chumbani na siwezi kuchanganya wanaume sababu najua sio mhanyaji,” asema Liza.

Anasema uhusiano wao umeimarika baada ya kutalikiana. “Huwa anatimizia watoto mahitaji yote na siku yangu ya kuzaliwa alininunulia zawadi ambayo sijawahi kupata katika maisha yangu. Aliniambia alifanya hivyo kama rafiki. Mwaka jana alikuwa mgonjwa na nilimshughulikia hadi akapona,” asema Liza.

Wataalamu wa masuala ya mapenzi na ndoa wanasema kuwa watu wanaweza kuchangamkiana baada ya talaka kwa kuzingatia sababu zilizowafanya kuvunja ndoa.

“Inawezekana wanandoa waliotalikiana kuwa na uhusiano hata wa kimapenzi. Inategemea sababu ya kuvunja ndoa yao. Ikiwa hawakutalikiana kwa sababu ya dhuluma na uzinifu, ni rahisi wao kuchangamkiana na hata kulishana uroda,” asema Doreen Nameme wa shirika la Big Hearts jijini Nairobi.

Nameme anasema kuna watu wanaopapia kutaliki wachumba wao na baadaye wanagundua walikosea.

“Ndio sababu huwa nashauri watu kuchukua muda kutafakari kabla ya kuamua kutaliki wachumba wao. Kuna tofauti zinazoweza kutatuliwa kupitia mazungumzo badala ya talaka,” asema Nameme.

Kulingana na Pasta Lois Gichohi wa Kanisa la Glory Assembly jijini Nairobi, baadhi ya watu huwa wanataliki wachumba wao kwa kuiga wengine. “Kuna watu wanataliki wachumba wao kwa kuwa marafiki zao walifanya hivyo au walisikia walifanya hivyo. Baadaye wanagundua kwamba walikosea. Talaka inafaa kuwa kwa misingi ya kidini na kisheria ambayo imethibitishwa kikamilifu. Kwa maoni yangu, wanaotalikiana sio wanandoa tena na wakifanya mapenzi huwa wanatenda dhambi kwa kuwa sio mume na mke,” asema Gichohi.

Mshauri huyu anasema kukiwa na mawasiliano miongoni mwa wanaotalikiana, ni rahisi kwao kulishana uroda.

“Hii inawezekana ikiwa hawakuachana kwa sababu ya uzinifu au dhuluma,” asema.

Jessica Mwelu, mwanadada mwenye umri wa miaka 34 anasema hawezi kumfungulia mumewe wa zamani mzinga kwa sababu alikuwa akimpiga na kumtesa sana.

“Huwa sitaki kumuona kwa macho yangu. Niliyopitia katika mikono yake kwa miaka sita ni Mungu tu anajua,” asema.

Lakini David Okello anasema yeye na aliyekuwa mkewe huwa wanalishana tunda kila mwezi miaka mitatu baada ya kutalikiana rasmi.

“Alikuja kwangu baada ya mwezi mmoja na akaniambia hawezi kupatia mwanamume mwingine mwili wake nikiwa hai. Mimi sijawahi kuwa na mwanamke mwingine katika maisha yangu na ingawa alinitaliki kutokana na presha kutoka kwa wakwe, tungali tunaburudishana,” asema Okello.

Pasta Gichohi anasema kwamba watu waliowahi kulala kitanda kimoja sio rahisi kunyimana uroda licha ya kutengana. “Ndio sababu tunashauri watu kuvumiliana. Kuna presha nyingi zinazochangia talaka siku hizi ambazo zinaweza kuepukwa kupitia ushauri nasaha kutoka kwa wataalamu waliohitimu,” asema.

Nameme anasema kuna hatari ya watalaka kulishana uroda hasa ikiwa mmoja wa wahusika ameoa au kuolewa. “Itakuwa ni kuzini na pia inaweza kuvuruga maisha ambayo mtu alitamani baada ya kupata talaka. Lakini ikiwa hakuna aliyeoa au kuolewa na kwa hiari ya kila mmoja, wanaweza kulishana uroda katika mazingira salama,” asema.

You can share this post!

KAMAU: Uhuru ajaribu kurejesha utulivu katika ngome yake

FUNGUKA: ‘Navutiwa na kijinyanya’