Na WYCLIFFE NYABERI
NAIBU Rais William Ruto, sasa amesema hana haja kulipwa deni la kisiasa na mtu yeyote.
Mwishoni mwa wiki, Rais Uhuru Kenyatta akiwa katika Ikulu ya Sagana alikuwa amepuuzilia mbali viongozi wanaomshinikiza kumuunga mkono Dkt Ruto kwa urais 2022, akisema deni lake ni kwa Wakenya pekee.
Akiongea jana katika kanisa la Enoosaen Maranatha, lilio Transmara, Kaunti ya Narok, Dkt Ruto aliunga mkono kauli ya Rais akasema waliahidi kuwatumikia Wakenya walipokuwa wakiwaomba kura zao.
‘Nilipoamua kumuunga ndugu yangu Uhuru Kenyatta mwaka 2013 sikuwa na fikra za ukabila hata kidogo. Nilimuunga mkono kwa kuwa niliamini katika maono yetu yaliyooana ya kuwafanyia Wakenya maendeleo,’ akasema.
Akirejelea kauli maarufu ya Rais kwamba angetawala kwa kipindi cha mwongo mmoja na kisha ampishe naibu wake kwa kipindi kingine cha miaka kumi, Ruto alisema kuwa Rais alitamka hayo kwa hiari yake na bila kupewa masharti yoyote wala kushurutishwa.
Alisisitiza ana maono na sera nzuri ambazo yuko tayari kuzunguka kote nchini kuwauzia Wakenya akiingia kwa kinyang’nyiro cha urais 2022.