• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 9:12 AM
Wakazi wafurahia corona kupunguza ulevi vijijini

Wakazi wafurahia corona kupunguza ulevi vijijini

NA KALUME KAZUNGU

WAKAZI wa mitaa ya Wiyoni na Mararani, kisiwani Lamu wamesifu kipindi cha janga la Covid-19 kwa kusaidia kupunguza fujo zilizokuwa zikishuhudiwa kutoka kwa walevi maeneo hayo.

Mara nyingi wakazi wa mitaa hiyo miwili walikuwa wakijitokeza kulalamikia makelele na fujo zilizokuwa zikichangiwa na kukithiri kwa mangwe kwenye mitaa yao, hali ambayo ilikuwa ikiwakosesha usingizi.

Wakazi waliambia Taifa Leo Jumatatu kwamba idadi ya walevi wanaozuru mangwe maeneo yao imepungua pakubwa ilhali baadhi ya mangwe zimefifia n ahata kufungwa.

Wakazi pia waliisifu serikali kupitia idara ya usalama kwa kuendeleza misako ya mara kwa mara ambayo imesaidia pakubwa kupunguza au kuzifunga mangwe kwenye mitaa mbalimbali ya Lamu.

Bi Halima Yusuf alisema siku za hivi karibuni wamekuwa wakilala bila kusumbuliwa na makelele au vita vya walevi kinyume na miaka iliyopita.

“Tunashukuru kwamba kipindi hiki cha Korona kimechangia baadhi ya mangwe kufungwa eneo hili. Kila mara tulikuwa tukiamsha au hata kukosa kulala kabisa kutokana na zahama za walevi ambao walikuwa wakiimba au kupigana,” akasema Bi Yusuf.

Karisa Charo ambaye ni mkazi wa Mararani alisema tangu Covid-19 ianze Machi mwaka jana, mtaa wao umegeuka kuwa mtulivu kwani walevi wengi hupendelea kunywa mchana pekee ilhali usiku wanakimbilia kwenye nyumba zao.

Aliiomba serikali kutoondoa kafyu, akisisitiza kuwa imegenyorosha tabia za wengi ambao usiku na mchana walikuwa wakibugia mtindi.

“Hapa Mararani ilikuwa ni kelele mchana kurwa na usiku kucha. Tunafurahia kafyu ya Covid-19. Imewatia woga walevi wengi. Wao hupendelea kunywa masaa machache na pia mchana pekee. Usiku mangwe zinafungwa mapema na watu kwenda kulala kinyume na awali ambapo makelele ya walevi yalikuwa yakiendelea usiku kucha hapa,” akasema Bw Charo.

Wakazi walisema sheria za Covid-19, ikiwemo kafyu pia imesaidia kuleta nidhamu miongoni mwa wanaume na vijana ambao hawakuwa wakiripoti nyumbani mapema.

“Mume wangu alikuwa akishinda na kukesha nje kula miraa na kunywa pombe. Nafurahi kwamba tangu Covid-19 kuanza, yeye amekuwa akifika nyumbani mapema n ahata kujukumikia masuala mengine ya kifamilia,” akasema Bi Sidi Kithi.

You can share this post!

Maaskofu wafunguka kuhusu corona Tanzania, wataka wananchi...

TANZIA: Simeon Nyachae afariki