• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 AM
Joho ashauriwa kuhusu urais 2022

Joho ashauriwa kuhusu urais 2022

Na WINNIE ATIEO

GAVANA wa Mombasa Hassan Joho ametakiwa kuwapatanisha viongozi wote wa Pwani kabla hajatangaza azma yake ya kuwania urais mwaka ujao.

Mbunge wa Kisauni, Ali Mbogo alimsihi Bw Joho kuhakikisha umoja wa Pwani umepatikana kwanza ili aweze kupata uungwaji mkono.

“Kama kinara wa ODM Raila Odinga atakubali kumwachia nafasi Bw Joho na kuunga mkono azma yake, itakuwa jambo bora sana kwa wapwani. Lakini ni sharti Bw Joho na magavana wenza Salim Mvurya (Kwale) na Amason Kingi (Kilifi) wakae chini na kutafuta atakayepeperusha bendera ya urais eneo la Pwani. Lazima wazungumze lugha moja,” akasema Bw Mbogo.

Pia alimtaka Bw Joho afanye kikao na wanasiasa wote wa Mombasa, hasa wabunge, ili waweze kumsaidia katika safari yake ya uongozi.

“Lazima wakubaliane ni nani atawania urais ili Wapwani wote wampigie debe. Bw Joho huwezi kutembea peke yako kama wataka urais. Shirikiana na wabunge Mohammed Ali (Nyali), Mishi Mboko (Likoni), Omar Mwinyi (Changamwe), Badi Twalib (Jomvu) na Abdulswamad Nassir (Mvita) na MCA wa Mombasa,” akasema.

Wiki iliyopita, Gavana Kingi alisema hivi karibuni atatangaza mkondo ambao Pwani itafuata kisiasa.

Bw Kingi amekuwa akipigania kuanzishwa kwa chama cha Pwani, ambacho alisisitiza kiko katika mkondo wa mwisho.

You can share this post!

‘Simba’ wa Kisii kukumbukwa kwa kunguruma

Uhuru sasa awategemea Raila, Kalonzo na Mudavadi kuvumisha...