• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:55 PM
CHARLES WASONGA: Serikali ikome kuhujumu vyama vya kutetea wafanyakazi

CHARLES WASONGA: Serikali ikome kuhujumu vyama vya kutetea wafanyakazi

Na CHARLES WASONGA

NI haki ya wafanyakazi kote ulimwenguni kujiunga na vyama vya kutetea masilahi yao kama vile nyongeza ya mishahara na marupurupu na kuboreshwa kwa mazingira yao ya kikazi.

Hii ndio maana kipengele cha 41 cha Katiba ya sasa kinalinda haki ya mwajiriwa kuunda au kujiunga na chama cha kutetea masilahi yake sawa na kushiriki majadiliano na waajiri wao kuhusiana na masuala hayo.

Sheria ya Leba ya 1997 pia inatambua wajibu wa vyama hivyo katika kujadiliana na waajiri kuhusiana na masuala ya ajira.

Kwa hivyo, juhudi zinazoendeshwa wakati huu na serikali kuu na zile za kaunti kuhujumu na kulemaza vyama vya kutetea masilahi ya wafanyakazi ni kinyume cha Katiba na sheria hii muhimu.

Baada ya kung’amua kuwa inafanikiwa kuua Chama cha kitaifa cha Walimu (Knut) kwa kutumia Tume ya Kuajiri Walimu (TSC), serikali kuu sasa inashirikiana na Baraza la Magavana Nchini (CoG) kuangamiza vyama vya kutetea masilahi ya wahudumu wa afya.

Waziri wa Afya Mutahi Kagwe na mwenzake wa Utumishi wa Umma Profesa Margaret Kobia, wamekubaliana na CoG kwamba kama waajiri wa wahudumu wa afya, hawatakuwa wakiwasilisha michango ya wafanyakazi hawa kwa vyama husika, kila mwezi, kama ilivyo ada.

Hii ina maana kuwa vyama kama vile, Chama cha kutetea masilahi ya madaktari (KMPDU), kile cha kutetea wauguzi (KNUN), kile cha matatibu (KUCO) miongoni mwa vingine vitalazimika kusubiri wanachama kuwasilisha michango yao baada ya kupokea mishahara.

Kuna uwezekano mkubwa kuwa wengi wa wanachama hawatawasilisha michango yao kivyao, hali ambayo itatumbukiza vyama hivyo katika lindi la changamoto za kifedha.

Hali hii bila shaka, itachangia vyama hivyo kukosa makali ya kutetea masilahi ya wahudumu wa afya ipasavyo na hatimaye kusambaratika. Knut inahujumiwa na TSC kwa namna hii kando na wanachama wake kunyimwa nyongeza ya mishahara na manufaa mengineyo.

Matokeo yake ni kwamba, Knut imepoteza uwezo wa kifedha wa kufadhili shughuli zake katika matawi kando na wanachama wake wengi kuhama na kujiunga na Chama cha Kutetea Masilahi ya Walimu wa Shule za Upili na Vyuo vya Kadri (KUPPET).

Naona hali kama hii ikikumba vyama vya kutetea masilahi ya wahudumu wa afya na kuvifanya kuwa butu kiasi cha kushindwa kutekeleza majukumu yao.

Matokeo yake ni kwamba huenda wahudumu wa afya wanaofanya kazi katika hospitali za umma watajiuzulu na kujiunga na zile za kibinafsi au kusaka ajira katika mataifa ya ng’ambo.

Atakayeumia ni mwananchi wa kawaida ambaye hutegemea huduma za afya zinatotolewa na hospitali za umma kwa kushindwa kumudu gharama ya juu ya huduma hizo katika hospitali za kibinafsi au zile za ughaibuni.

Serikali Kuu na CoG zimekome kuhujumu vyama vya kutetea masilahi ya wahudumu wa afya.

You can share this post!

FAUSTINE NGILA: Vita vya Iran, Israel visizuie ukuaji wa...

Matamshi ya Arati yalinikera, pikipiki yangu ilichomwa...