Na DERICK LUVEGA
KIONGOZI wa chama cha Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi amesema hatarajii kukabidhiwa uongozi wa nchi hii na kuwataka wapinzani wake wajiandae kwa makabiliano makali kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022.
Akihutubu katika kaunti ya Vihiga Bw Mudavadi, aliwaambia wafuasi wake kinaga ubaga kwamba “yuko tayari kupambana kufa kupona katika kinyang’anyiro cha urais.”
Bw Mudavadi alionyesha wazi wazi kuwa yeye hahitaji kuteuliwa mbali amehitimu katika kila njia kuwania kiti cha Urais wa nchi hii.
Bw Mudavadi alisema yuko tayari kujitetea kwa wananchi na kuwashauri wanaomuunga mkono wasitilie maanani mihemko ya kisiasa inayosambazwa huku na kule.
“Wakati umewadia uongozi wa nchi hii uhame kutoka kwa Uhuru hadi kwa Mudavadi. Tusisubiri kukabidhiwa,” alisema Bw Mudavadi.
Matamshi hayo ya Bw Mudavadi yamejiri siku chache baada ya vyombo vya habari kuashiria kwamba ndiye anayependelewa na Ikulu kutawazwa kumridhi Rais Uhuru Kenyatta.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kutokana na matamshi ya Rais Kenyatta wakati wa mazishi ya mama yake Bw Mudavadi Januari 9, 2020 kwamba wakati umewadia kabila nyingine kutwaa uongozi mbali na Wagikuyu na Wakalenjin.
Matamshi hayo yalitafsiriwa na wadau kuwa Rais Kenyatta amemteua mrithi wake.
Jana Bw Mudavadi aliwasihi wanaomuunga mkono kwa mbio za atakayemrithi Bw Kenyatta wajiandae barabara.
Alikuwa akiwahutubia waombolezaji wakati wa mazishi ya aliyekuwa kamishna katika tume ya uchaguzi iliyovunjwa (ECK) Francis Chogo