• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
MIIBA TELE MBELE YA UHURU

MIIBA TELE MBELE YA UHURU

Na MWANGI MUIRURI

JUHUDI za Rais Uhuru Kenyatta kutuliza uhasama dhidi ya mipango anayonuia kutimiza kabla ya kuustaafu hapo 2022, zinazidi kugonga mwamba.

Rais amekuwa akisisitiza kuwa nia yake ni kuhakikisha kuna amani atakapoondoka mamlakani, ametimiza maendeleo yatakayoboresha maisha ya wananchi, na vilevile kufanikisha marekebisho ya katiba kupitia Mpango wa Maridhiano (BBI).

Wiki iliyopita, Rais alijizatiti kushawishi ngome yake ya Mlima Kenya iungane naye katika safari hii nzima kwani eneo hilo limekumbwa na misukosuko tele ya kisiasa tangu alipoweka muafaka na Kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga mnamo 2018.

Hata hivyo, ziara hiyo iliyojumuisha mikutano na viongozi katika Ikulu ya Sagana, haijafanikisha mengi kwani anazidi kurushiwa makombora na wanasiasa wanaokosoa mienendo yake.

Licha ya rais kusisitiza kuwa ni lazima wanasiasa walio ndani ya chama tawala cha Jubilee wakome siasa za mapema kuhusu 2022, kampeni hizo zingali zinaendelea kuvutia umati mkubwa wa watu.

Vilevile, pingamizi dhidi ya Mpango wa Maridhiano (BBI) zingali zinaendelezwa na wandani wake wa zamani akiwemo Naibu Rais William Ruto.

Cheche za maneno anazorushiwa ndizo zilizomfanya kulalamika majuzi akitaka wanasiasa “waheshimiane”.

“Kufanya kampeni kwetu huzuia namna gani tingatinga za kutekeleza maendeleo mashinani? Tukiwa katika harambee kwa kanisa, huwa tunazima namna gani mawaziri kutoa kandarasi za kimaendeleo ili Wakenya wapate maendeleo?” akauliza mbunge wa Kiharu, Ndindi Nyoro.

Lakini watetezi wa Rais wanasema hatababaishwa kamwe na wapinzani wake bali ataendelea kutekeleza wajibu wake. Kulingana na Mbunge Maalumu, Bw Maina Kamanda, ambaye ni mmoja wa wandani wa Rais, kiongozi wa taifa alikuwa akitatizika sana katika awamu yake ya kwanza ya uongozi.

Bw Kamanda alieleza kuwa Rais amefanikiwa kutekeleza mambo mengi ambayo hayangewezekana tangu alipoungana na Bw Odinga.

“Mmesikia mtu akisema Baba (Bw Odinga) alikuja kuharibu Jubilee. Kama si huyu mzee… Uhuru alikuwa na taabu sana. Si mnaona kitambi ya Uhuru imekuwa sawasawa? Hii ni kwa sababu ya Baba,” akasema jana alipokuwa katika Kaunti ya Turkana.

Rais Uhuru Kenyatta. PICHA/ MAKTABA

Bw Kamanda alisema wanaopinga misimamo ya Rais ni bora waondoke kwa upole waachie wengine nafasi ya kushirikiana na serikali kujenga taifa.

Mbunge wa Bahati, Bw Kimani Ngunjiri alisema hali itatulizwa tu ikiwa Rais atajitolea kwa Jubilee jinsi ilivyochaguliwa kuanzia 2013, akubali kuwa kuna deni la kisiasa kati ya wafuasi wake na wale wa Dkt Ruto na hatimaye wote katika undugu ndani ya mrengo mmoja wa kisiasa wapange kuhusu kura ya 2022 pamoja “bila ukora wa kusalitiana.”

Tayari, kumeibuka vyama kadhaa ambavyo vinatishia kusambaratisha umoja wa Mlima Kenya ambao umekuwepo kwa miaka mingi kisiasa.

Kinara wa chama cha The Service Party (TSP), Bw Mwangi Kiunjuri, alidai kuwa mienendo ya Rais inafaa kulaumiwa kwa vikwazo anavyokumbana navyo.

“Kile hatutakubali ni anavyotusukuma pembeni na hatimaye awe ndiye pekee ana ruhusa ya kutuharibia majina. Akiniharibia jina hata mimi nitamjibu,” akasisitiza waziri huyo wa zamani wa Kilimo.

Msimamo sawa na huu ulitolewa na Mbunge wa Mathira Bw Rigathi Gachagua ambaye alisema Rais ndiye aliyepoteza mwelekeo kisiasa.

“Tumekuwa naye katika safari yake ya siasa kwa zaidi ya miaka 20 lakini katika siku za hivi karibuni amekuwa wa kupotoshwa, atuchukie na kutuadhibu pasipo sababu kiasi kwamba inatubidi tujitetee,” akasema.

Kulingana na kinara wa Narc Kenya, Bi Martha Karua, itakuwa vyema kama Rais Kenyatta atatulia jinsi mtangulizi wake Mwai Kibaki alivyofanya hadi akastaafu.

You can share this post!

Elfsborg ya Joseph Okumu yang’aria Helsingborg msimu...

Akamatwa baada ya kuua mkewe na watoto wake wawili