• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:30 PM
UDAKU: Boateng achepukiwa sawa tu na afanyavyo!

UDAKU: Boateng achepukiwa sawa tu na afanyavyo!

Na CHRIS ADUNGO

BEKI wa Bayern Munich na timu ya taifa ya Ujerumani, Jerome Boateng, 32, ametemana rasmi na kipusa Kasia Lenhardt miezi 15 baada ya mwanamitindo huyo kuchanja chale za kudumu zenye maandishi ya jina la Boateng kwenye maziwa yake.

Kwa mujibu wa gazeti la Bild nchini Ujerumani, Kasia, 25, alihusika kwenye ajali ya barabarani mnamo Januari 5 akiendesha gari la Boateng. Baada ya kufanyiwa vipimo vya afya katika hospitali ya Berlin Charite, ilibainika kwamba kichuna huyo alikuwa mlevi chakari.

Boateng alihoji kwamba jumbe alizozipata kwenye simu ya mchumba wake huyo zilidhihirisha kwamba alikuwa ametoka kuonana na mpango wake wa kando aliyeshiriki naye ulevi na pia kuchovya asali mzingani mwa Kasia.

“Yangu na Kasia yamekwisha kuanzia leo. Japo yasikitisha, nahisi kwamba hii ni hatua bora. Naomba msamaha kutoka kwa wote nitakaowakosea kwa maamuzi yangu hayo, hasa demu wangu wa zamani Rebecca na watoto wangu. Najihurumia hapa nilipo. Kasia ni tapeli,” akaandika Boateng kwenye mtandao wake wa Instagram.

Kasia alijibu ujumbe huo wa Boateng kwa kupakia picha yao ya pamoja na kuandika: “Nami nimeshindwa na uongo wako. Una jicho kali la nje lililonichochea kufanya hayo unayodhani nilifanya. Nitafichua yote hivi karibuni. Sijawahi kuhisi kudanganyika na kutumika hivi. Nipeni muda mashabiki wangu. Nitarejea kwa fujo na Boateng hatapenda kitakachompata.”

Mwanzoni mwa mwaka huu 2021, Boateng alijipata katikati ya vita vikali baina ya vichuna wawili waliokuwa wakipigania penzi lake motomoto.

Mwanamitindo Rebecca Silvera alimchemkia Kasia mtandaoni na kumwita ‘fisi-jike’ lililompokonya dume lake wakati ambapo walikuwa pua na mdomo kufunga pingu za maisha.

Kupitia Instagram, Rebecca alifichua jinsi alivyokuwa akiwasiliana na Boateng mara kwa mara huku akimfichulia rafikiye Kasia hatua zote alizokuwa akipiga katika safari yake ya kimapenzi na mwanasoka huyo mshindi wa Kombe la Dunia na taji la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

“Ambalo sikujua ni kwamba Kasia naye alikuwa amesalitika kihisia kwa Boateng. Alifahamu kila kitu kuhusu uhusiano wetu hata nyakati ambapo nilikuwa nimekosana na mwanasoka huyo,” akatanguliza Rebecca.

“Kumbe rafiki niliyemwamini alikuwa fisi-jike! Kasia alimwendea Boateng na kumzuzua kwa mapenzi! Bila shaka alielewa jinsi ya kumteka kwa sababu nilikwisha kumfichulia kila kitu – hata namna ambavyo Boateng alipenda sana apakuliwe vya chumbani,” akaandika Rebecca.

Akihojiwa awali na gazeti la The Sun, Boateng alimtaka Rebecca kumkoma kabisa kadri alivyopanga kumvisha Kasia pete ya uchumba na kumfanya wake wa halali.

Kwa upande wake, Kasia alimtaka Rebecca amsamehe na kumtakia kila heri wakati anapojiandaa kuanza kumfyatulia Boateng watoto.

“Rebecca, haikuwa nia yangu kukusononesha, ila nilishindwa kabisa kujizuia kumpa Boateng ufunguo wa mzinga wangu wa asali. Nilivutiwa sana na simulizi ulizokuwa ukinipa kumhusu nami nikachochewa kumpa tunda adokoe. Nimemwonjesha asali, na ajabu ni kwamba amepania kujenga mzinga!” akaandika Kasia.

Rebecca alijibu ujumbe huo hivi: “Nawatakia uhusiano mwema lakini ujue sitakuachia Boateng wangu hivyo tu. Inaniuma sana!”

Boateng aliwahi kufunga pingu za maisha na kichuna Sherin Senler mnamo Machi 2010 baada ya kuchumbiana naye kwa kipindi cha miaka minne. Walijaliwa pacha wa kike Soley na Lamia mnamo Machi 2011. Hata hivyo, walitengana mwaka mmoja baadaye kutokana na jicho la nje la Boateng.

aliyeanza kuchovya kwa Rebecca kisha Kasia. Ingawa sogora huyo aliwasha upya mwenge wa mapenzi kati yake na Sherin mnamo Julai 2015, uhusiano wao haukudumu baada ya sogora huyo kuanza kumtambalia mwanamitindo maarufu raia wa Ujerumani, Gina-Lisa Lohfink.

You can share this post!

Bunge la Kaunti ya Kiambu kujadili ripoti ya BBI

ONYANGO: Uhuru atufafanulie zaidi kuhusu wizi wa mabilioni