• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Siasa za matusi ni hatari – Mukhisa Kituyi

Siasa za matusi ni hatari – Mukhisa Kituyi

Na CHARLES WASONGA

ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa Kuhusu Biashara na Maendeleo (UNCTAD) Mukhisa Kituyi amewaonya wanasiasa dhidi ya kuendesha siasa za chuki zenye madhara ya ufufuzi wa uchumi.

Kwenye kikao chake cha kwanza na wanahabari Jumapili katika hoteli moja jijini Nairobi Dkt Kituyi amesema inawezekana kwa wanasiasa kutofautiana kwa njia ya heshima bila yao wao kurushiana cheche za matusi kama ambavyo wamekuwa wakifanya katika siku za hivi karibuni.

“Ni makosa kwa baadhi ya wanasiasa nchini kuchukua tofauti za kisiasa kama sababu ya wao kurushiana matusi hadharani kwani hii itawaogofya wawekezaji. Tuendeshe siasa za ustaarabu na heshima,” akasema Dkt Kituyi.

Wanasiasa katika kambi za Naibu Rais William Ruto na kiongozi wa ODM Raila Odinga katika siku za hivi karibuni wamekuwa wakitoa matamshi ya chuki, uchochezi na matusi katika majukwaa mbalimbali.

Hii ni kwenye harakati za wao kutetea misimamo yao ya kisiasa, wandani wa Dkt Ruto wakipinga BBI na wale wa Odinga wakiunga mkono mchakato huo wa marekebisho ya katiba.

Dkt Kituyi, ambaye zamani alikuwa Mbunge wa Kimilili na Waziri wa Biashara, alisema akipatiwa nafasi ya kumrithi Rais Uhuru Kenyatta kama Rais wa tano wa Kenya, atatumia ujuzi wake katika Umoja wa Mataifa (UN) kubadilisha maisha ya Wakenya.

Hata hivyo, aliungama kuwa anafahamu changamoto zinazomsubiri katika azma yake ya kutimiza ndoto hiyo.

“Naingia kwenye kinyang’anyiro cha urais nikifahamu kuwa kuna wengine ambao walianza safari hii mapema kuniliko. Lakini ningependa kuwahakikisha Wakenya kuwa wakinipa nafasi hii, nitaleta mawazo mapya uongozini kutokana na tajriba kubwa ambayo nimepata katika mida ya kimataifa,” akasema Dkt Kituyi mwenye umri wa miaka 65.

Katibu huyo mkuu UNCTAD aliyejiuzulu juzi, alisema kuwa ataelekea nyumbani kwao Bungoma kusaka “baraka kutoka kwa wazee na kufanya mashauriano zaidi” kabla ya kurejea Nairobi kuzindua rasmi kampeni zake za urais.

You can share this post!

UIGIZAJI: Harriet Kwamboka Charles aamini anacho kipaji cha...

Kibarua cha Gor Mahia kukabiliana na mikosi ya ugenini soka...