• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:36 PM
Hofu wanafunzi hawavai maski wakiwa shuleni

Hofu wanafunzi hawavai maski wakiwa shuleni

Na WAANDISHI WETU

WANAFUNZI wameacha kuvalia barakoa wakiwa shuleni au kuzivaa visivyo hatua ambayo inawaweka katika hatari ya kuambukizwa virusi vya corona.

Baadhi yao wanabadilishana barakoa zao. Jambo hili limeanza kuwatia wasiwasi wazazi.Hii ni tabia ya kushtua wakati ambao takwimu za wizara ya afya zinaonyesha kuwa katika muda wa wiki mbili sasa, kiwango cha maambukizi ya corona kinaongezeka nchini.

Uchunguzi wa Taifa Leo umeonyesha kuwa baadhi ya wanafunzi pia wanavaa barakoa chini ya kidefu na wengine wanabadilisha zao.Wataalamu wa afya wanasema tabia hii inaweza kusambaza virusi.

Kulingana na kituo cha kudhibiti kusambaa kwa magonjwa (CDC), kuambia wanafunzi wavae barakoa si sawa na wao kuzivaa kwa njia inayofaa.

“Barakoa inafaa kufunika pua na mdomo vyema hadi chini ya kidefu. Watoto wanaweza kuvaa barakoa moja siku nzima isipokuwa ipate unyevu au kuchafuka. Hata hivyo, wote wanafaa kuwa na barakoa mbili na wazazi wanafaa kununua barakoa maalumu kwa watoto,” ripoti ya kituo hicho inasema.

Ripoti hiyo inaeleza kwamba watoto wanaweza kupata dalili zisizo kali za corona au kutopata dalili na kwa hivyo kuna haja yao kuvalia barakoa wakiwa karibu na watu.

Mnamo Alhamisi mwanafunzi wa shule ya msingi katika kaunti ya Nairobi alienda nyumbani akivalia barakoa ya mwanafunzi mwingine.

Alipoulizwa kiini, alimwambia mama yake kwamba alibadilishana na rafiki yake ambaye rangi ya barakoa yake ilikuwa ya kuvutia kuliko yake.Katika baadhi ya shule, wanafunzi wa chekechea wanapolala baada ya chamcha, huwa wanaweka barakoa zao katika eneo moja na wanapoamka, huwa wanachukua yoyote na kuvaa.

Katika uchunguzi, Taifa Leo ilibaini kuwa wanafunzi wakiwa katika mabasi ya shule asubuhi na jioni wengi wao huwa wanazivaa chini ya kidefu.Hali hii inashuhudiwa kote nchini kutokana kauli za wazazi katika mitandao ya kijamii wakilalamika kwamba watoto wao wanabadilishana barakoa wakiwa shuleni.

“Kwa nini kila wakati mtoto wangu akitoka shuleni huwa anavaa barakoa ya rangi tofuati na anayotoka nayo nyumbani asubuhi, wanabadilishana lini barakoa zao? Walimu wanafaa kuwa makini,” mzazi kwa jina Elizabeth aliandika kwenye mtandao wa kijamii.

Mzazi mwingine kwa jina Nancy alisema kwamba mwanawe huwa anarudi kutoka shule bila barakoa. “Huwa hana habari alipoipoteza na wapi,” alisema.

“Watoto wanafaa kuvaa barakoa wakipanda mabasi ya shule, wakiingia na kutoka shuleni na wakiwa madarasani,” ripoti ya CDC inahimiza.Shirika la Afya Ulimwenguni linahimiza shule zitumie mbinu tofauti kuhakikisha wanafunzi wanazoea kuvaa barakoa.

“Shule zinafaa kuweka mabango ya kuonyesha jinsi ya kuvaa barakoa vyema katika madarasa na maeneo mbalimbali kama vile kumbi za shule,” linasema shirika hilo.

Wakakti huo huo, idara ya afya katika kaunti ya Mombasa imeanza kutoa chanjo ya homa ambayo ilikuwa imesitishwa kufuatia maambukizi ya corona.

Ripoti za Angela Oketch, Maureen Ongala na Wachira Mwangi

You can share this post!

TAHARIRI: Tumbo lisiongoze maamuzi ya BBI

TANZIA: Seneta Haji afariki