• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 6:25 PM
Joho alipa Sh1m kuwania tiketi ya urais ya ODM kabla ya Raila

Joho alipa Sh1m kuwania tiketi ya urais ya ODM kabla ya Raila

Na JUSTUS OCHIENG

Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho ndiye mwanasiasa pekee ambaye kufikia sasa amewasilisha ombi la kusaka tiketi ya ODM ili kuwania Urais 2022 huku zikiwa zimesalia siku 10 pekee makataa yaliyowekwa yakamilike.

Kinara wa ODM Raila Odinga na Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya ambao pia wameonyesha azma ya kuingia ikulu kupitia chama hicho mhapo 2022, bado hawajawasilisha maombi yao huku makataa ya Februari 26 yakinukia.

Katibu Mkuu wa ODM, Bw Edwin Sifuna jana alifichua kwamba ODM imepokea ombi la Bw Joho lakini akasema hafahamu chochote iwapo Mabw Odinga na Oparanya watawasilisha maombi yao kabla ya muda uliowekwa.

“Tumepokea ombi la Gavana Joho na tunatarajia maombi ya wawaniaji wengine yataendelea kumiminika kabla ya makataa kutimia. Hatujasikia kutoka kwa wawaniaji wengine ila tuna matarajio watatii wito huo siku chache zinazokuja,” akasema Bw Sifuna.

Bw Odinga amekuwa kimya kuhusu iwapo atakuwa debeni 2022 au la na sasa amebaki na siku 10 ili ifahamike iwapo atatafuta kurithi kiti cha urais baada ya Rais Uhuru Kenyatta kustaafu mwakani.

Gavana Oparanya katika mahojiano na Taifa Leo hapo awali alithibitisha kuwa yuko kiny’ang’anyironi kusaka tiketi ya ODM ili awanie urais kwa mara ya kwanza.

Mabw Oparanya na Joho wanahudumu vipindi vyao vya pili kama magavana na katiba haiwaruhusu watetee viti hivyo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Uchaguzi wa ODM, Bi Catherine Mumma alikataa kuzungumzia kuhusu iwapo Bw Odinga atawasilisha jina lake, akisema suala hilo litakuwa wazi baada ya Februari 26.

“Wale ambao wana azma ya kuwania urais lazima wawasilishe majina yao kufikia Februari 26. Unaweza kutuma maombi baada ya makataa hayo iwapo muda huo utarefushwa. Baada ya kupokea majina, tutaanza mchakato wa ukaguzi,” akasema Bi Mumma.

ODM inatarajiwa kuandaa uchaguzi wa wanachama mashinani kuanzia mwezi ujao kisha wajumbe watakaoshinda watapewa nafasi ya kumchagua mpeperushaji bendera wa chama hicho.

iwapo maombi ya Urais yatatumwa na zaidi ya mwaniaji mmoja.

Katibu wa ODM Timothy Bosire alieleza Taifa Leo kuwa chama hicho hakitamfungia nje Bw Odinga au wawaniaji wengine wenye nia ya kukitumia kuwania urais 2022.

Naye wabunge Mark Nyamita (Uriri) na Elisha Odhiambo (Gem) walisema Odinga ndiye mwaniaji pekee wa urais wanayemtambua kutokana na umaarufu wake wa kisiasa kote nchini.

“Urais wa Raila haupo kwenye msingi wa iwapo atatuma maombi au la. Lazima atakuwa debeni la sivyo tutaigura ODM na kuachana na siasa kabisa. Ni yeye pekee atakayevunia chama chetu ushindi na mwenye uwezo wa kuunganisha taifa hili,” akasema Bw Nyamita.

You can share this post!

Mungu ni mkuu, asema mkurugenzi baada ya kuondolewa...

Mwenyekiti wa BBI azikwa bila cheche za siasa