• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 7:55 AM
Yaibuka uwanja wa ndege hutegemea vibuyu kuchota maji

Yaibuka uwanja wa ndege hutegemea vibuyu kuchota maji

Na KALUME KAZUNGU

WAFANYAKAZI katika uwanja wa ndege wa Manda, Kaunti ya Lamu hulazimika kuchota maji kwa vibuyu kutoka visimani kwa matumizi uwanjani humo unaokumbwa na uhaba mkubwa wa maji.

Uchunguzi uliofanywa na Taifa Leo umebaini kuwa wafanyakazi kwenye uwanja huo wa ndege hutumia mitungi kusafirisha maji kwa mashua kutoka visima vya Shella hadi kwenye uwanja huo wa ndege wa Manda ambao ni umbali wa karibu kilomita 10.

Baadhi ya wafanyakazi waliozungumza na wanahabari na kudinda kutaja majina yao kwa kuhofia kufutwa kazi walisema tatizo hilo la maji lilianza karibu miezi miwili unusu iliyopita.

‘Mara nyingi tunalazimika kuamka alfajiri na kwenda kujaza maji kwa mitungi katika visima vya Shella. Baadaye tunaisafirisha kwa boti au mashua hadi kwenye uwanja wa ndege wa Manda,” akasema mmoja wa vibarua.

Vibarua kwenye uwanja wa ndege wa Manda wakisambaza maji vyooni na sehemu zingine. Uhaba wa maji unaendelea kukumba eneo hilo. PICHA/KALUME KAZUNGU

Wasafiri waliohojiwa pia walikiri kukumbwa na kipindi kigumu kila wanaposhuka uwanjani humo hasa tangu tatizo la maji lilipoanza kushuhudiwa.

Akijibu suala hilo, Mkurugenzi Mkuu wa Halmashauri ya Viwanja vya Ndege (KAA) Ukanda wa Pwani, Peter Wafula, alisema uhaba wa maji kwenye uwanja huo huenda umechangiwa na kupungua kwa kiwango cha maji kinachosambazwa kwenye kisiwa cha Manda na Bodi ya Kusambaza Maji ya Lamu (LAWASCO) hasa tangu msimu wa kiangazi ulipoanza eneo hilo.

Bw Wafula, aidha alisema uhaba huo wa maji haujaathiri pakubwa shughuli za kila siku katika uwanja huo wa ndege kwani wamekuwa wakitumia mbinu mbadala, ikiwemo kusafirisha maji kwa boti kutoka eneo la Shella hadi Manda kila mara.

Naye Meneja wa LAWASCO, Kimani Wainaina, alitaja kukauka kwa baadhi ya visima kwenye bwawa la Shella hasa tangu msimu wa kiangazi ulipoanza Lamu kuwa changizo kuu linalopelekea kiwango cha maji kinachosambazwa sehemu nyingi za Lamu, ikiwemo Uwanja wa Manda kupungua.

Mara nyingi wamekuwa wakiepuka kutumia vyoo kwani baadhi ni vichafu. PICHA/ KALUME KAZUNGU

Bw Wainaina pia alitaja hitilafu ya umeme ambayo imekuwa ikishuhudiwa mara kwa mara eneo la Lamu katika siku za hivi karibuni kuwa sababu mojawapo ya maji kukosa kusambazwa inavyostahili katika miji na vijiji vya Lamu.

‘Pia ningesihi KAA kukarabati mabomba yake ya maji kutoka Shella hadi uwanja wa ndege wa Manda kwani ni ya zamani na yanaathiri kiwango cha maji kinachosambazwa eneo hilo,” akasema Bw Wainaina.

Ali Zubeir alisema mara nyingi wamekuwa wakiepuka kutumia vyoo kwani baadhi ni vichafu. ‘Kuna vingine hata vimefungwa kutokana na ukosefu wa maji. Hiyo inamaanisha ukitaka kutumia choo lazima usubiri mwenzako,’ akasema Bw Zuberi.

You can share this post!

BBI sasa yafaulu kunasa kaunti za kwanza Bondeni

Pigo kwa chama cha UDA Machakos baada ya wandani kutoroka