• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Pigo kwa chama cha UDA Machakos baada ya wandani kutoroka

Pigo kwa chama cha UDA Machakos baada ya wandani kutoroka

NA PIUS MAUNDU

CHAMA cha United Democratic Alliance (UDA), kimepata pigo katika uchaguzi mdogo wa useneta wa Machakos baada ya kutorokwa na wanasiasa wanne waliotegemewa katika kampeni.

Aliyekuwa Naibu Gavana, Bernard Kiala na wanasiasa wengine watatu wamebadilisha msimamo wao wa kumuunga mkono mwaniaji wa UDA, Bw Urbanus Muthama Ngengele katika uchaguzi huo wa Machi 18.

Bw Kiala na watatu hao ambao ni diwani wa zamani wa Matungulu Magharibi, Bi Magdalene Ndawa na wanasiasa Stephen Muthuka na Rita Ndung ni kati ya wawaniaji 13 ambao walikosa nafasi ya kutwaa tiketi ya chama hicho kinachohusishwa na Naibu Rais William Ruto, baada ya Bw Ngengele kukumbatiwa bila mchujo wowote kuandaliwa.Walisema hakuwa na imani na kura ya maoni iliyotumika kumpokeza Bw Ngengele tiketi ya chama moja kwa moja.

‘Natangaza kujiondoa katika kampeni za Urbanus Muthama Ngengele kuhusiana na uchaguzi mdogo wa useneta. Mimi bado ni mwanachama wa UDA na ninaunga mkono sera ya kuwainua Wakenya wa mapato madogo kiuchumi,’ akasema Bw Kiala kupitia taarifa.

Jana, Bw Kiala alihudhuria mkutano wa chama cha Wiper hali inayoashiria kuwa atamuunga mkono mgombeaji wa chama hicho Agnes Kavindu Muthama.

‘Nashauriana na wafuasi wangu ili kutathmini mwaniaji ambaye tutampigia kura mnamo Machi 18,’ akaongeza.

Kiti hicho kilisalia wazi baada ya mauti ya Boniface Kabaka mnamo Disemba mwaka jana.Wawaniaji wengine wanaomezea mate useneta huo ni John Mutua Katuku (Maendeleo Chap Chap Party), Dkt John Musingi (Muungano Party), Stanley Masai Muindi (Party of Economic Democracy), Edward Musembi Otto (Ford Asili) na Simeon Kioko Kitheka (Grand Dream Development Party).Wengine ni Sebastian Nzau, Jonathan Maweu na Francis Musembi ambao ni wawaniaji huru.

You can share this post!

Yaibuka uwanja wa ndege hutegemea vibuyu kuchota maji

CHARLES WASONGA: Wabunge wanaodaiwa kupokea hela za mafuta...