• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 AM
WANDERI KAMAU: Tujinasue sasa kutoka kwa mfumo wa kibepari

WANDERI KAMAU: Tujinasue sasa kutoka kwa mfumo wa kibepari

Na WANDERI KAMAU

MDAHALO unaoendelea katika ulingo wa siasa nchini kuhusu watu matajiri na wale maskini, ni timio la onyo tulilopewa mapema mara tu baada ya Kenya kujinyakulia uhuru.

Wasomi na wanasiasa walioshabikia mfumo wa ukomunisti au ujamaa, walitoa maonyo kuwa hiyo ndiyo njia iliyofaa zaidi kuiepushia Kenya uwepo wa matabaka hayo mawili—mabwanyenye na walalahoi.

Hata hivyo, viongozi waliokuwa serikalini waliwaona kama maadui na ‘kuwanyamazisha’ mara moja ili “kutoivuruga nchi.” Baadhi ya watu hao ni mwandishi Ngugi wa Thiong’o, wanasiasa Jaramogi Oginga Odinga, Bildad Kaggia, Pio Gama Pinto, JM Kariuki kati ya wengine.

Katika karibu maandishi yake yote, Ngugi amekuwa miongoni mwa waandishi wachache ambao wamejitokeza wazi kuonya na kukashifu mfumo wa kibepari.

Tangu zamani, amekuwa akikita msimamo wake kuhusu mwoano mkubwa uliopo kati ya ujamaa na mfumo wa kimaisha walioishi Waafrika kabla ya uhuru.

Ni mawazo aliyoyarejelea kwenye vitabu kama ‘Weep Not, Child’ (Usilie Mpenzi Wangu), ‘The Trial of Dedan Kimathi ‘(Hukumu ya Shujaa Dedan Kimathi), Matigari ma Njiruungi (Waliobaki Baada ya Vita), ‘Ngaahika Ndeenda’ (Nitaoa Nikipenda) kati ya vingine.

Kwa mfano, katika novela ‘Usilie Mpenzi Wangu’, Ngugi anachora taswira kuhusu vile ubepari ulivyozua pengo na uadui mkubwa kati ya Wazungu na Waafrika.Chini ya mfumo huo, Wazungu walionekana kama ‘miungu’ nao Waafrika kama watumwa.

Ni mfumo ulioonekana kukita mizizi sana kiasi kwamba, Waafrika wenyewe walikuwa wamekubali kuwa wao ni “binadamu wa hadhi ya chini” ikilinganishwa na Wazungu.

Ni katika mazingira hayo ambapo wafanyakazi wa Kiafrika walizoea kuwaita waajiri wao Wazungu kama “lords” (mkubwa wangu) huku nao Wazungu wakiwaita Waafrika “boi” (mtumwa).

Hadi sasa, wazee wachache waliobaki huwa wanarejelea ugumu waliopitia chini ya wazungu, kwani waliwachukulia kuwa duni hata kuliko mbwa wao!Jaramogi aliendeleza mawazo hayo kwenye tawasifu yake ‘Not Yet Freedom’ (Hatujapata Uhuru), Kaggia kwenye kitabu ‘Roots of Freedom: 1921-1963’ (Mizizi ya Ukombozi) huku Kariuki akinakili mawazo yake kwenye tawasifu yake ‘Mau Mau Detainee’ (Mau Mau Kizuizini).

Ujumbe wao mkuu kwenye vitabu hivyo ni kwamba ubepari ungegeuka kuwa chemichemi ya mapigano ya kitabaka, ambayo ni hatari zaidi hata kuliko ghasia za kikabila.

Kinaya ni kuwa, licha yao kuhangaishwa, kudhulumiwa na kunyamazishwa na serikali ya Mzee Jomo Kenyatta, laana hiyo ndiyo inayotuandama sasa.Leo, Kenya ni miongoni mwa nchi zinazoorodheshwa kuwa na pengo kubwa sana kati ya watu matajiri na wale maskini.

Ni kwa hilo ambapo wanasiasa kama Naibu Rais William Ruto wameanza kukita kampeni zao kwenye juhudi za “kuziba” pengo hilo.Ukweli ni kuwa, mkasa huu ni mwiba wa kujidunga.

Tulionywa mapema na wale walioona hatari ya mfumo wa kibepari. Tuliwapuuza na kutupilia mbali mawazo yao. Tuliwaona kama watu duni, wasioelewa chochote.Majuto ni mjukuu. Wakati umefika tuanze kutathmini uzito wa tabiri zao.

[email protected]

You can share this post!

Wanajeshi wakataa kupokea chanjo ya corona

Raia waadhimisha miaka 10 ya kung’oa utawala wa Gaddafi