• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 9:50 AM
Shule za bweni zipigwe marufuku – Kuppet

Shule za bweni zipigwe marufuku – Kuppet

GEORGE SAYAGIE na GERALD BWISA

CHAMA cha kutetea Masilahi ya Walimu wa Shule za Upili na Vyuo (KUPPET) jana kiliendeleza wito wake wa kutaka shule za mabweni zipigwe marufuku.

Mwenyekiti wa chama hicho Omboko Milemba alisema hiyo ndio mojawapo ya njia za kukomesha visa vya fujo na utovu wa nidhamu shule.Akiongea baada ya kushuhudia uchaguzi wa tawi la Narok la Kuppet, Bw Milemba pia aliitaka serikali kusambaza vifaa kwa usawa shuleni ili kusawazisha viwango vya elimu.

“Shule za mabweni zinafaa kupigwa marufuku na vifaa viwe katika shule zote ili mwanafunzi wa hapa Narok aweze kufaidi sawa na mwenzake katika Shule ya Upili ya Alliance,” akasema Milemba ambaye pia ni Mbunge wa Emuhaya.

Alisema hayo wakati ambapo visa vya wanafunzi kuteketeza shule vimekuwa vikiongezeka, wakilenga mabweniBw Milemba pia aliitaka Tume ya Huduma za Walimu (TSC) kupandisha vyeo walimu wote waliohitimu huku akilitaka bunge kutenga fedha nyingi kwa tume hiyo.

“TSC pia inahitaji fedha zaidi ili iweze kuajiri walimu watakaotekeleza Mtaala Mpya wa Umilisi na Utendaji (CBC),” akasema.

Wakati huo huo, polisi katika kaunti ya Trans Nzoia wanawazuilia wanafunzi 14 kwa tuhuma za kuteketeza mabweni mawili wakitaka waruhusiwe kwenda nyumbani kuleta karo.

Kulingana na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Wasichana ya Heart Girls iliyoko kaunti ndogo ya Saboti, Bi Rosemary Bor, alipata habari saa sita za usiku kwamba mabweni mawili yalikuwa yakichomeka..

“Hapo kwa hapo nilipasha habari maafisa wa polisi. Walimu, wanafunzi na wanakijiji walijaribu kuzima moto huo lakini ukawalemea,” akasema Bi Bor.

Wazima moto kutoka serikali ya kaunti ya Trans Nzoia na maafisa wa polisi ndio walifaulu kuuzima moto huo.Malazi na mali nyingi ya wanafunzi iliharibiwa kabisa.

Katika kaunti ya Makueni, wanafunzi wa Shule ya Upili ya Wavulana ya Makueni walimjeruhi mwalimu wao mkuuu Raphael Katana, walipozua fujo Ijumaa usiku.Kufuatia kisa hicho shule hiyo imewaagiza wanafunzi wote 258 wa kidato cha nne waende nyumbani kwa wiki mbili kutoka nafasi kwa uchunguzi kuhusiana na kisa hicho, akasema Bw Katana.

You can share this post!

Wajomvu sasa wataka warudishiwe ardhi yao

JAMVI: Mrengo wa Weta, Musalia, Kalonzo, Moi watia Raila,...