• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 3:17 PM
Mutua, Kibwana sasa waunga BBI

Mutua, Kibwana sasa waunga BBI

Na PIUS MAUNDU

MAGAVANA Dkt Alfred Mutua (Machakos) na Profesa Kivutha Kibwana (Makueni) Jumatatu walionekana kubadili msimamo na kuyarai mabunge ya kaunti za Ukambani yapitishe mswada wa marekebisho ya katiba (BBI).

Wawili hao walikuwa mstari wa mbele kupinga BBI, wakisema huu si wakati muafaka wa kukumbatia marekebisho ya katiba na pia wakidai wanasiasa wameteka mchakato wa kuvumisha ripoti hiyo bila kuwahusisha raia.

Hata hivyo, jana, walikutana na madiwani 20 kutoka Machakos na Makueni mjini Machakos ambapo kwa kauli moja walitangaza kuwa mabunge ya kaunti za Ukambani yatapitisha BBI.

“Nimesikia sauti ya wananchi kuhusu ushirikishaji wa umma kwenye mswada wa BBI. Raia walifurahishwa na nyongeza ya asilimia 35 kwa kaunti badala ya asilimia 15 ya sasa. Naheshimu maoni ya raia na pia nawaomba madiwani wayazingatie na kupitisha mswada huo,” akasema Profesa Kibwana.

Kwa upande wake, Dkt Mutua aliwataka raia wapitishe BBI katika kura ya maoni inayotarajiwa ila akasema magavana wa kaunti husika na viongozi waliochaguliwa hawafai kutelekezwa kwenye mchakato huo.

You can share this post!

Bobi Wine sasa ainua mikono, amwachia Mungu

Kidero akemea wanaovuruga mikutano