• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Washukiwa wawili Thika wanaswa na lita 4,000 za pombe haramu

Washukiwa wawili Thika wanaswa na lita 4,000 za pombe haramu

Na LAWRENCE ONGARO

WASHUKIWA wawili wamenaswa na maafisa wa upelezi wakitengeneza pombe katika jumba moja mjini Thika.

Hii ni baada ya wakazi wa kijiji cha Kisii mjini Thika kupiga ripoti kwa maafisa wa polisi ambao waliandamana na makachero ambao waliwatia nguvuni.

Wawili hao ilidaiwa wamepakana na shule moja ya msingi katika eneo hilo.

Maafisa hao waliovamia eneo hilo mnamo Jumatatu walinasa lita 4,000 za pombe ambayo ilikuwa imepakiwa kwa chupa na kuwekwa kwa katoni kadha.

Kamande wa polisi wa Thika Magharibi, Bi Beatrice Kiraguri, alisema washukiwa hao wamekuwa wakiendesha biashara hiyo kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa.

“Tumepata habari ya kwamba pombe hiyo hutengezwa usiku na kupakiwa kwa katoni ili isafirishwe hadi jijini Nairobi,” alisema Bi Kiraguri.

Naibu kamishna wa Thika Magharibi aliyeandamana na maafisa wakuu wa polisi, Bw Mbogo Mathioya, alisema ni hatia kubwa kwa mtu yeyote kuendesha biashara ya pombe karibu na eneo la shule.

“Wale ambao wanaendesha biashara hiyo wajue ya kwamba siku zao zimewadia,” alisema Bw Mathioya.

Alisema wawili hao watahojiwa zaidi kabla ya kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka.

Hata hivyo washukiwa hao walijitetea vikali wakisema kuwa wao wanaendesha biashara halali na tayari wana leseni inayowaruhusu kuendesha biashara hiyo.

Lakini malalamishi yao yalikosa kutiliwa maanani na maafisa wa usalama.

Bw Mathioya alisema maafisa wa upelezi wataendelea na msako kuona ya kwamba watu hawaendeshi biashara haramu katika kaunti ndogo ya Thika.

Aliwapongeza wananchi kwa kuwa mstari wa mbele kuwatambua watu wanaotenda maovu miongoni mwao na baadaye kupiga ripoti kwa maafisa wa usalama.

You can share this post!

Shalom Yassets yawatandikia vijana zulia la upenyo

Jepchirchir aongezwa kwenye orodha wa wawakilishi wa Kenya...