• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
GWIJI WA WIKI: Musau Muia

GWIJI WA WIKI: Musau Muia

Na CHRIS ADUNGO

MWENYEZI Mungu alipokuumba, alikupangia ramani ya maisha yako. Kila siku fanya jambo ambalo litakupigisha hatua ya kusonga mbele katika barabara ya kutafuta ufanisi.

Kuishi ni matendo. Uzembe si mzuri. Zohali ni nyumba ya njaa. Taa ya mafanikio yako huwaka wakati unapojituma na kujizatiti katika shughuli za kila siku. Guru Ustadh Wallah Bin Wallah husema, “Huwezi kuushika wakati na kuufungia usisonge. Usipoenda na wakati utaachwa na wakati. Wakati ndio mkate!”

Ipande mbegu ya ufanisi kila siku ya maisha yako na mavuno yatakuwa mazuri na mengi ajabu. Kusema kweli, huwezi ukapanda mahindi kisha utarajie kuvuna kahawa! Mtu huvuna anachokipanda. Ukipanda na kupalilia vyema, bila shaka utapata tabasamu ya milele. Jitume sana leo ili kesho ufurahie matunda ya jasho lako!

Ukitaka kufikia kileleta cha mafanikio, nyenyekea na uwastahi wanadamu wengine. Unyenyekevu ni mbolea katika kufanikiwa kwa mtu. Usiwe mwenye magwaji na magumashi. Heri watu wakuone mjinga kutokana na unyenyekevu wako.

Huu ndio ushauri wa Bw Musau Muia – mwandishi chipukizi wa Isimu na Fasihi ambaye kwa sasa ni mwalimu wa Kiswahili katika Shule ya Upili ya Mukaa Boys, Kaunti ya Makueni.

MAISHA YA AWALI

Musau alizaliwa Agosti 8, 1993 kijijini Mang’elete, Makueni. Ni mwana wa katikati katika familia ya Bw James Muia na Bi Ann Mutee.

Amesomea katika shule tatu tofauti za msingi kwa sababu ya uhamisho wa kikazi wa baba yake. Alianzia safari hiyo ya elimu katika Shule ya Msingi ya Mang’elete kati ya 2000 na 2005 kabla ya kujiunga na Shule ya Msingi ya Mtito-Andei mnamo 2006.

Baadaye, alijiunga na Shule ya Msingi ya Emali, Makueni. Huko ndiko alikofanyia Mtihani wa Kitaifa wa Darasa la Nane (KCPE) mwishoni mwa 2007.

Msukumo wa kukipenda Kiswahili ulizidishwa na vitabu vya ‘Kiswahili Mufti’ ambavyo vimeandikwa na Guru Ustadh Wallah Bin Wallah. Vitabu hivyo vilimpa ilhamu ya kukichangamkia Kiswahili kutokana na maelezo bora yaliyomo.

Kwa hakika, vitabu hivyo vilichangia zaidi ya asilimia 80 katika alama 96 alizopata katika KCPE Kiswahili. Alifaulu vyema na kupata fursa ya kusomea katika Shule ya Upili ya Mukaa Boys mnamo 2008.

Ni wakati akiwa Mukaa ambapo aliboresha kiwango chake cha umilisi wa Kiswahili baada ya kuhimizwa pakubwa na walimu wake. Bw Kaula alimfaa sana kwa nasaha zake aula. Aidha ndiye aliyeidhinisha ombi la Musau la kuanzisha Jopo la Kiswahili (kwa sasa ni Chama cha Kiswahili cha Mukaa). Idhini hiyo ilimpa nafasi ya kuwa Kaimu Mwenyekiti wa chama hicho.

“Bw Kaula alinichochea pakubwa kukipenda Kiswahili. Alipanda ndani yangu mbegu zilizootesha utashi na kariha ya kukichapukia Kiswahili. Alijitolea kunielekeza kwa ari na idili.”

Nasaha za mwalimu mkuu, Bw Francis Mutunga Mutua, zilimpa msukumo chanya katika kuyatambua na kuyachambua maisha.

Kuna kauli ya mwalimu mkuu anayoikumbuka hadi leo. Kwamba, “Failure is a situation, never a person. Notice the difference between what happens when a man says to himself that he failed three times and what happens when he says he is a failure.”

Maneno hayo yalimkosha kwelikweli na kumfumbua macho kabisa.

Bw Kaula ambaye sasa ni Naibu wa Mwalimu Mkuu anayesimamia masuala ya akademia, pia alichangia ufanisi wa Musau. Kauli yake kwamba, “ivitukaniaa kitindioni” iliamsha ari na hamu ya kujizatiti ili aweze kutimiza ndoto zake.

Kauli hii ya Bw Kau ina maana kwamba wanafunzi wanapoenda shuleni, huwa ni wengi na wanafungiwa katika zizi moja (shule). Wanapoendesha shughuli zao shuleni, kuna wale wanaofanikiwa na kunao pia wanaokosa kufaulu kutegemea namna wanavyoutumia muda wao.

Uongozi katika Jopo la Kiswahili ulimpa Musau fursa maridhawa ya kuitafitia lugha ya Kiswahili. Usikivu, umakini na heshima ya wanafunzi wenzake ni miongoni mwa mambo yaliyomshajiisha sana.

USOMI NA UTAALAMU

Musau alijiunga na Chuo Kikuu cha Egerton (Bewa Kuu) mnamo Septemba 2012. Alipania kufanya shahada ya Isimu – Kiswahili na Kiingereza lakini akaarifiwa kwamba isingewezekana na akashauriwa aende Ujerumani kunakofanywa kozi hiyo.

Alipewa michepuo kadhaa ya masomo achague anaotaka. Kwa sababu ya utashi wake wa kusomea Kiswahili, aliishia kufanya shahada ya ualimu (Kiswahili na Dini).

Akiwa chuoni, alijiunga na Chama cha Kiswahili cha Egerton (CHAKIE). Mnamo 2013, aliingia katika uongozi wa CHAKIE baada ya kuchaguliwa kuwa Katibu.

Mwanzoni mwa mwaka wa 2015, alichaguliwa kuwa Katibu Mtendaji wa CHAWAKAMA-Kenya. Wadhifa huo wa ulimpa motisha zaidi ya kukichapukia Kiswahili.

Musau amehudhuria makongamano mengi ya Kiswahili ndani na nje ya nchi. Mnamo 2013, alihudhuria Kongamano la Kimataifa la Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili katika Vyuo Vikuu vya Afrika Mashariki (CHAWAKAMA) jijini Kigali, Rwanda.

Mnamo 2016, alihudhuria Kongamano la Kimataifa la CHAWAKAMA nchini Zanzibar katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Mnamo Machi, 2020 aliwapeleka wanachama wa Chama cha Kiswahili cha Mukaa (CHAKIMU) katika Kituo cha WASTA, Matasia, Ngong ambako walijifunza mengi kutoka kwa Guru Ustadh Wallah Bin Wallah. Kwa mujibu wa Musau, nasaha za Wallah Bin Wallah zimechangia pakubwa kuboresha matokeo ya mtihani na kuimarisha nidhamu miongoni mwa wanafunzi wa Shule ya Upili ya Mukaa Boys.

Baada ya kufuzu na shahada ya kwanza, Musau alianza kufundisha Kiswahili na somo la Dini katika Shule ya Upili ya Mukaa Boys mnamo 2016 na ndiye mlezi wa CHAKIMU. Musau kwa sasa ni mwanafunzi wa shahada ya uzamili katika Chuo Kikuu cha Nairobi.

UANDISHI

Musau ni mwandishi chipukizi wa kazi za Kiswahili. Ndoto yake ya uandishi ilichipuza alipokuwa mwanafunzi wa shule ya upili. Mara si chache aliwahi kushiriki mashindano mbalimbali akiwa katika shule ya upili na kuwapiku wenzake wa vidato vya juu.

Jambo hilo likawa kiini cha msukumo wake wa kujitosa katika ulingo wa uandishi wa vitabu. Kwa sasa anaandikia kampuni ya Spearsharp Educational Publishers vitabu vya Kiswahili kwa minajili ya Mtaala Mpya wa Umilisi (CBC). Isitoshe, ana miswada ya kazi mbili ambazo anaamini zitachapishwa mwishoni mwa mwaka huu: ‘Usaili Sahili wa Sarufi’ na ‘Utu na Ubinadamu’. Musau ana imani kwamba nakala hizi zikichapishwa, zitabadilisha pakubwa sura ya ujifunzaji na ufundishaji wa Kiswahili ndani na nje ya Kenya.

JIVUNIO

Musau anaivulia kofia familia yake ambayo imekuwa ikimpa kila sababu ya kujikaza kisabuni. Anastahi sana mkewe Bi Victoria Ndanu ambaye amekuwa akimhimiza sana kukichangamkia Kiswahili.

Isitoshe, anajivunia kuwa na wanafunzi ambao wamekuwa kiini cha mapenzi ya dhati aliyo nayo kwa kazi yake.

You can share this post!

Kwani kuliendaje?

Bayern Munich waponda Lazio 4-1 kwenye mkondo wa kwanza wa...