• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Wadau walia utalii unaendelea kusambaratika nchini

Wadau walia utalii unaendelea kusambaratika nchini

Na WINNIE ATIENO

SEKTA ya Utalii eneo la Pwani inazidi kudorora huku janga la corona likiendelea kuathiri biashara nchini.

Wawekezaji wa utalii wanasema wanaendelea kukadiria hasara kubwa kufuatia janga hilo na kuzorota kwa uchumi.

Kufikia sasa hoteli za pwani zina asilimia 20 ya wageni huku msimu wa chini wa wageni ukiingia baada ya mwaka mgumu wa utalii wa 2020 kufuatia janga hilo ambalo lililemaza utalii na usafiri.

Wawekezaji hao waliokuwa wakitegemea watalii wa humu nchini baada ya wale wa kimataifa kususia kusafiri kufuatia janga hilo wamebakia bila wageni katika hoteli zao.

Juhudi za serikali kuokoa sekta hiyo pia inakadiriwa zinagonga mwamba baada ya wawekezaji wengi kususia mkopo wa Sh3 bilioni ili kujinasua. Wanadai kuwa serikali imeweka sheria kali za mkopo huo.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa Wawekezaji wa Utalii nchini Bw Mohamed Hersi, Afisa Mkuu wa Muungano wa Watalii Pwani Julius Owino na Afisa Mkuu wa Muungano wa Wafanyakazi wa Hoteli nchini tawi la Pwani, Dkt Sam Ikwaye, walisema wageni wa humu nchini ndio wamekuwa wakipiga jeki sekta hiyo.

“Tunaishi siku baada ya siku, hatujui siku zetu za usoni. Awali tulidhani chanjo ya corona ndio sulu

hisho lakini tunaendelea kushuhudia maafa hususan Uingereza ambapo mambo yanazidi kuwa magumu. Nchi nyingi ambazo ni soko letu la utalii zimefungwa tena sababu ya maambukizi ya corona,” alisema Bw Hersi.

Alisema hatima ya janga haijulikani suala linaloendelea kutishia utalii.

Hata hivyo, kutokuwa na uhakika kumewalazimisha wamiliki wa hoteli kuanza kubuni mbinu maalum ili kushawishi soko la ndani na vivutio vingine. Wamiliki hao wanapunguza ada za hoteli.

“Hoteli zinatoa viwango vya chini kabisa ambavyo havijawahi kufanyika katika historia kutokana na janga hili. Hata hivyo tangu Januari, vituo hivyo vimebaki tupu,” akasema Bw Owino.

Utalii ni uti wa mgongo wa uchumi wa ukanda wa Pwani unaoajiri wafanyakazi 12,800. Lakini kwa sasa nusu ya wafanyakazi hao wanafanya kazi kwa mshahara wa asilimia 50 kwa sababu ya kudorora kwa uchumi.

Mei mwaka jana, Rais Uhuru Kenyatta alizindua mkopo wa Sh3 bilioni ili wawekezaji wa utalii wajinasue kutoka kwa changamoto.

Hata hivyo, wawekezaji wengi bado hawajachukua mkopo huo.

Wawekezaji hao wanaitaka serikali kupunguza kodi na gharama za ada ya umeme wakisema iko juu.

Eneo la Pwani lilipewa mgao mkubwa wa mkopo huo wa Sh1.8 bilioni kati ya Sh3 bilioni sababu uchumi wake unategemea utalii.

Wamiliki wa hoteli wanapewa mkopo huo kwa kiwango cha riba ya asilimia tano. Bw Owino alieleza wasiwasi wake kwamba endapo wamiliki wa hoteli hawatochukua mikopo hiyo huenda ikaregeshwa serikali kuu.

“Tunatoka katika kipindi kigumu lakini lazima tung’ang’ane. Tunaisihi serikali kupunguza ushuru ambao bado uko juu kutoka asilimia 16 hadi 14. Serikali inafaa kufutilia mbali kodi za mwaka 2020 sababu hakukuwa na biashara,” alisisitiza Bw Owino.

Hata hivyo wawekezaji hao wana matumaini kwamaba sekta hiyo itafufuka kwanzia likizo ya Agosti. Walisema asilimia 80 ya faida wanazopata kwenye biashara hizo huregea kwenye mahoteli ili kuendesha sekta hiyo.

Dkt Ikwaye alisema utalii wa ndani huendeshwa kulingana na kalenda ya elimu.

“Lakini badala ya wakenya kusafiri watu wanafikiria karo za shule, janga hili limeathiri soko letu. Serikali inaa ibuni sheria zitakazoongoza ufufuaji wa sekta hii. Lakini mfumo unaochukuliwa na serikali utalemaza utalii sababu ya kuinyima wizara fedha za kuuuza Kenya,” alisisitiza Dkt Ikwaye.

You can share this post!

Alipata tenda ya Sh1.3bn miezi 2 baada ya kusajili kampuni

Covid: Serikali yakana wandani wa Museveni walipewa chanjo