• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
Kampeni za Matungu zaingia hatua ya lala-salama

Kampeni za Matungu zaingia hatua ya lala-salama

Na SHABAN MAKOKHA

WAGOMBEAJI wa ubunge katika eneo la Matungu, Kaunti ya Kakamega, wako katika harakati za mwisho za kampeni zao, zinapobaki siku tano pekee kabla ya uchaguzi huo kufanyika.

Katika harakati za kuhakikisha wamefanikisha juhudi zao, wagombeaji hao wamekuwa wakifika katika kila pembe ya eneobunge hilo kuwarai wenyeji kuwapigia kura.

Vyama vya kisiasa vimewatuma wabunge wao kufanya mikutano ya kuwapigia debe wawaniaji wake, huku wagombeaji wakifanya kampeni za nyumba hadi nyumba.

Seneta Cleophas Malala wa Kakamega na mbunge Titus Khamala (Lurambi) wanaongoza kampeni za mwaniaji wa chama cha ANC, Bw Peter Nabulindo, anayetajwa kuwa miongoni mwa washindani wakuu.

Kampeni za Bw Nabulindo zimepigwa jeki na uwepo wa kiongozi wa chama hicho, Bw Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka (Wiper), Gideon Moi (Kanu) na Moses Wetang’ula (Ford-Kenya).

Mwanzoni mwa mwezi huu, Bw Nabulindo aliwaambia washindani wake “kujitayarisha kwa kivumbi”.

Wabunge Oscar Sudi (Kapseret), Mwambu Mabonga (Bumula), John Waluke (Sirisia), Didmus Barasa (Kimilili), Fred Kapondi (Mt Elgon) na Malulu Injendi (Malava) wameungana na aliyekuwa Seneta wa Kakamega, Boni Khalwale, mbunge Benjamin Washiali (Mumias Mashariki) na aliyekuwa Waziri wa Michezo, Rashid Echesa, kumpigia debe Bw Alex Lanya, anayewania kwa chama cha UDA.

Hapo Alhamisi, msafara wa UDA ulifanya mikutano katika kijiji cha Sayangwe wadi ya Koyonzo, eneo la Ebubambula katika wadi ya Mayoni na eneo la Makunda katika wadi ya Kholera. Wabunge hao waliwaomba wenyeji kumchagua Bw Lanya, Machi 4.

Msafara wa ANC ulikuwa katika kijiji cha Shibanze (wadi ya Kholera), eneo la Itete katika wadi ya Koyonzo na eneo la Ngaire.

Chama cha ODM kimeanza mkakati mpya, kwa kukutana na makundi mbalimbali katika eneo hilo. Mgombeaji wake ni David Were.

You can share this post!

Amri Balala, Keter wafike mbele ya Seneti

Faki ataka nakala za BBI kwa Kiswahili