• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:30 PM
Man-City wacharaza West Ham United na kuanza kunusia taji la EPL

Man-City wacharaza West Ham United na kuanza kunusia taji la EPL

Na MASHIRIKA

MANCHESTER City waliendeleza ubabe wao katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa kuwapepeta West Ham United 2-1 katika mchuano uliwawezesha kufikisha rekodi ya kushinda mechi 20 mfululizo.

Chini ya kocha Pep Guardiola, Man-City kwa sasa wanajivunia alama 62 huku pengo la pointi 13 likitamalaki kati yao na Manchester United na Leicester City watakaovaana na Chelsea na Arsenal mtawalia leo Jumapili.

Beki Ruben Dias aliwaweka Man-City uongozini katika dakika ya 30 kabla ya fowadi Michail Antonio kusawazishia West Ham mwishoni mwa kipindi cha pili. Goli la ushindi kwa upande wa Man-City lilijazwa kimiani na difenda John Stones katika dakika ya 68.

Bao hilo lililochangiwa na kiungo Riyad Mahrez, lilikuwa la nne kwa Stones kufungia waajiri wake katika kampeni za EPL msimu huu.

West Ham ya kocha David Moyes sasa wanashikilia nafasi ya nne kwa alama 45, nne zaidi kuliko mabingwa watetezi Liverpool ambao wana idadi sawa ya alama na Everton ya kocha Carlo Ancelotti.

Man-City kwa sasa hawajashindwa katika jumla ya mechi 27 na huenda wakaifikia rekodi yao ya awali ya kutoshindwa kwenye idadi kubwa zaidi ya mechi za EPL iwapo watawaangusha Wolves mnamo Machi 2, 2021.

West Ham walioagan kipute cha Kombe la FA msimu huu sasa watakuwa na pumziko la siku tisa kabla ya kuwaalika Leeds United ligini kwa gozi la EPL mnamo Machi 8, 2021.

MATOKEO YA EPL (Februari 27):

Man-City 2-1 West Ham

West Brom 1-0 Brighton

Leeds 0-1 Aston Villa

Newcastle 1-1 Wolves

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Juventus wakabwa koo na Verona katika Serie A

Bayern Munich wanyanyasa Cologne na kuendeleza ubabe wao...