• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Walimu sasa walia, wataka nyongeza mpya ya mshahara

Walimu sasa walia, wataka nyongeza mpya ya mshahara

Na ERIC MATARA

CHAMA cha walimU (Knut), kinataka Tume ya Huduma ya Walimu (TSC), kuharakisha mazungumzo kuhusu makubaliano ya pamoja (CBA), kuwawezesha walimu kuanza kupata mishahara mipya kuanzia Julai 1, 2021.

Katibu Mkuu wa chama hicho Wilson Sossion, aliyezungumza akiwa mjini Nakuru baada ya kukutana na walimu kutoka eneo la Rift Valley, alisema kwamba mkataba wa sasa utaisha Juni 30 na utekelezaji wa CBA mpya unafaa kuanza Julai 1 ilhali TSC haijakamilisha shughuli hiyo.

“Nilikutana na baraza la Knut la eneo la Rift Valley na tumejadili masuala kadhaa ikiwemo CBA inayokuja. Lililo wazi ni kuwa walimu wanafaa kuanza kupata mishahara mipya kuanzia Julai 1 kupitia mfumo ambao umejadiliwa vyema. Hili ndilo jukumu kuu la chama ,” alisema Bw Sossion baada ya mkutano uliofanyika katika hoteli ya Golden Palace Hotel.

Jumapili, Bw Sossion alikutana faraghani kwa takriban saa nne na wanachama wa tawi la Rift Valley la Knut ambapo walijadili masuala kadhaa ikiwa ni pamoja na CBA.Duru miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo zilifichulia Taifa Leo kwamba mazungumzo hayo pia yalihusu uchaguzi ujao wa chama hicho.

Mwenyekiti wa tawi la Rift Valley la Knut, Bw Maurice Barchok pia alitaka TSC kuidhinisha CBA haraka.“Kwa niaba ya walimu ninaowakilisha, ninahimiza TSC kuharakisha utekelezaji wa CBA kuhakikisha walimu wanaanza kupokea mishahara mipya kuanzia Julai 1,” alisema Bw Barchok.

Knut imekataa pendekezo la nyongeza ya mishahara la kati ya asilimia 16-32 ambalo TSC iliwasilisha kwa Tume ya Mishahara (SRC), ikisema haikuhusishwa.

You can share this post!

Klopp adai Liverpool yaweza kufanya makuu ligini licha ya...

Man U washindwa kupiga Chelsea