• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 6:45 PM
LEONARD ONYANGO: BBI ikipita mshahara wa wabunge ukatwe

LEONARD ONYANGO: BBI ikipita mshahara wa wabunge ukatwe

 

Na LEONARD ONYANGO

WATAALAMU wa masuala ya uchumi wanatabiri kuwa Wakenya watalazimika kutumia kati ya Sh60 milioni na Sh300 milioni zaidi kulipa mishahara na marupurupu ya wabunge na maseneta iwapo Mswada wa Mpango wa Maridhiano (BBI) utapitishwa na Wakenya katika kura ya maamuzi.

Kwa mujibu wa takwimu hizo zilizotolewa wiki iliyopita na Taasisi ya Masuala ya Kiuchumi (IEA), idadi ya wabunge katika Bunge la Kitaifa itaongezeka kutoka 349 wa sasa hadi 546 ambao wanapendekezwa na Mswada wa BBI.Iwapo Mswada wa BBI utapitishwa, idadi ya maseneta itaongezeka kutoka 67 hadi 94.

Kila seneta au mbunge hupokea jumla ya Sh1.3 milioni kila mwezi. Kiasi hicho kinajumuisha mshahara wa Sh710,000 na marupurupu ya aina mbalimbali kama vile Sh100,000 za kuketi kwenye vikao vya kamati, Sh150,000 maruprupu ya kuwajibika, Sh400,000 za usafiri na Sh15,000 za mawasiliano ya simu.

Kila mbunge au seneta hutengewa Sh10 milioni kwa ajili ya bima ya matibabu, mkopo wa Sh7 milioni za mkopo wa gari na Sh20 milioni za mkopo wa kununua nyumba.

Mikopo hii hulipwa katika muda wa miaka mitano.Fedha hizi za bwerere ndizo husukuma Wakenya, wakiwemo wasomi waliobobea katika nyanja mbalimbali, kujiuzulu na kujitosa kwenye siasa.

Ulafi wa kutaka mshahara huo mnono ndio husababisha wanasiasa kutumia hata mbinu chafu almuradi waingie Bungeni.Wabunge wa Kenya hulipwa mishahara minono kuliko baadhi ya marais wa nchi za Afrika.

Marais wa nchi kama vile Guinea, Cape Verde, Tunisia na Senegal hupokea mshahara wa chini ikilinganishwa na wabunge wa Kenya.

Waziri Mkuu

Mbali na kuongeza idadi ya wabunge na maseneta, Mswada wa BBI unapendekeza kuongezwa kwa afisi zilizopigwa marufuku na Katiba ya 2010, kama vile waziri mkuu, manaibu wa waziri mkuu na kiongozi rasmi wa upinzani.

Ni bayana kwamba Mswada wa BBI unalenga kuwatwika Wakenya mzigo mzito ambao tayari wanahangaika kutokana na uchumi mbovu ambao umesababisha ongezeko la ukosefu wa ajira, kuporomoka kwa viwanda kati ya changamoto nyinginezo.

Kwa mujibu wa Katiba, ulipofikia Mswada wa BBI haufai kufanyiwa mabadiliko Bungeni ili kupunguza idadi ya wabunge na maseneta.Hivyo basi kuna haja ya kupunguza mshahara na marupurupu ya wabunge na maafisa wengine wa serikali ili kuwaondolea Wakenya mzigo mzito wa kulipa ushuru endapo Mswada wa BBI utapitishwa.

Kwa mfano, hakuna haja ya kuwalipa wabunge marupurupu ya kuketi kwenye kamati ilhali hiyo ndiyo kazi waliyochaguliwa kufanya. Hakuna haja ya kulipa marupurupu ya usafiri ilhali wengi wa wabunge na maseneta hutumia fedha hizo katika kampeni zao za kibinafsi zisizo na manufaa kwa Wakenya.

You can share this post!

Maelfu waandamana kupinga ubaguzi katika utoaji wa chanjo...

WANTO WARUI: Likizo ya majuma 18 kwa wanafunzi wa gredi ya...