• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 7:55 AM
Tisho la baa la njaa kutokana na ukosefu wa maji Lamu

Tisho la baa la njaa kutokana na ukosefu wa maji Lamu

NA KALUME KAZUNGU

UHABA wa maji unaokumba vijiji vingi vya kaunti ya Lamu umewasukuma wakazi wengi kulala njaa katika wiki za hivi majuzi.

Wakazi wa vijiji vya Bar’goni, Kwasasi, Ingini, Kiangwe, Mokowe na maeneo mengine ya Lamu wamekuwa wakipitia kipindi kigumu cha kukosa maji na chakula, hasa baada ya visima walivyotegemea kupata maji kukauka kutokana na ukame unaoendelea eneo hilo.

Taifa Leo ilibaini kuwa wakazi wa vijiji kama vile Bar’goni,Ingini na Kwasasi kila siku hulazimika kutembea mwendo wa zaidi ya kilomita 20 kutafuta maji.

Mtungi mmoja wa lita 20 wa maji huuzwa kwa kati ya Sh 50 na Sh100. Akizungumza na wanahabari Jumapili, Mzee wa Nyumba Kumi kwenye Kijiji cha Bar’goni, Diza Doza, alisema wanalazimika kuishi bila chakula kutokana na ukosefu wa maji ya kupikia chakula hicho.

Bw Doza aliiomba serikali ya kaunti na ile ya kitaifa kufikiria kuwasambazia maji kwa kutumia malori kwani wanaumia.

“Kila siku tunaamka na kulala bila kuogakwani maji ni tatizo hapa. Isitoshe, baadhi ya familia hapa hulala kwa njaa kwa kukosa maji ya kutayarishia mlo. Kusafiri kutoka hapa Bar’goni hadi mjini Hindi ambako maji huuzwa ni karibu kilomita 21. Maji yenyewe yanauzwa kwa bei ghali. Serikali iangazie hali hii na kuitatua,” akasema Bw Doza.

Bi Amina Abuli akieleza mahangaiko wanayopitia kwa kukosa maji maeneo yao. PICHA/KALUME KAZUNGU

Bi Amina Abuli alisema wanawake na wanafunzi wa shule ndio huumia zaidi kwani hulazimika kuamka mapema na kutembea masafa marefu kwa miguu ili kutafuta maji.

Kulingana na Bi Abuli, idadi kubwa ya wanafunzi kijijini Bar’goni wamekuwa wakikwepa madarasa ili kuandamana na wazazi wao kutafuta maji kwenye maeneo ya mbali.

“Hapa Bar’goni visima vyote tulivyotegemea vilikauka kutokana na kiangazi. Kilichobakia ni uwe na uwezo wa kukodisha pikipiki kwa pesa nyingi ili ukanunuliwe maji Hindi. Ikiwa hilo huwezi kulimudu, basi unalazimika kutembea guu mosi guu pili hadi Hindi kununua maji. Wanafunzi hapa wamekuwa wakikosekana madarasani wakisaidia wazazi kutafuta maji,” akasema Bi Abuli.

Katikka mji wa Mokowe, wakazi wanalazimika kutumia maji ya chumvi kutoka kwa visima vilivyoko mkabala na ufuo wa Bahari Hindi eneo hilo.

Wakazi waliambia Taifa Leo kuwa huenda maji hayo yakawaathiri kiafya kwani mbali na kwamba ni ya chumvi, pia ni chafu.

Waliiomba serikali ya kaunti kupitia bodi ya kusambaza maji (LAWASCO) kuwaunganishia mifereji ya maji safi kwenye vijiji vyao ili wapumzike mahangaiko.

Kwa upande wake aidha, Afisa Mkurugenzi wa LAWASCO, Kimani Wainaina aliwashauri wakazi kujiandaa kushuhudia uhaba zaidi wa maji kote Lamu hasa msimu huu ambapo kiangazi kinaendelea kuathiri maeneo mengi nchini.

Bw Wainaina alisema karibu visima vitatu kwenye vyanzo vikuu vya maji ya Lamu eneo la Shella tayari vimekauka kufuatia ukame.

“Watu watarajie kushuhudia uhaba zaidi wa maji kwani kiangazi kinachoshuhudiwa kimechangia baadhi ya visima vya Shella kukauka. Hali ikiendelea hivi inamaanisha visima zaidi vitakauka, hivyo kuzidi kupunguza kiwango cha maji yanayosambazwa majumbani eneo hili,” akasema Bw Wainaina.

You can share this post!

MARY WANGARI: Juhudi za pamoja zinahitajika kufanikisha...

Kaizer Chiefs yapepetwa 4-0 na Wydad Athletic