• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 3:34 PM
Shinikizo mbunge amlipe mpenzi wa zamani Sh200,000 kila mwezi

Shinikizo mbunge amlipe mpenzi wa zamani Sh200,000 kila mwezi

Na RICHARD MUNGUTI

MBUNGE wa Ikolomani Bw Bernard Masaka Shinali ameshtakiwa na mwanamke anayedai alipata mtoto naye. Mwanamke huyo Ms Caroline Mutheu Mwakodi amedai kuwa Bw Shinali hamsaidii mtoto huyo.

Anaomba mahakama imshurutishe mwanasiasa huyo kulipa zaidi ya Sh200,000 kila mwezi kugharamia mahitaji ya mtoto huyo aliye na umri wa miaka mitano sasa.

Ripoti ya uchunguzi wa DNA iliyotolewa kortini imebaini kuwa Bw Shinali ndiye baba mtoto kibayolojia. Mahakama ya kuamua kesi za watoto Milimani Naironi imewaamuru mawakili wa Bw Shinali na Bi Mutheu wawasilishe kortini Machi 9 2021 ushahidi wao ndipo uamuzi utolewe.

Mawakili hao ni Bw Majanja Luseno anayemwakilisha Bw Shinali na Bw Katunga Mbuvi anayemwakilisha Mutheu. Katika ushahidi aliowasilisha kortini , Mutheu amedai kuwa walikuwa marafiki na Mbunge huyo hapo 2015 alipopachikwa mimba.

Mutheu, ameeleza kupitia kwa wakili Bw Mbuvi kuwa, alijaliwa kumzaa mvulana Mei 2016. Tangu ajifungue ameeleza kuwa mwanasiasa huyo alikoma kuwasaidia.

Bw Mbuvi anaomba mahakama imshurutishe Bw Shinali awe akimpa Mutheu zaidi ya Sh200,000 kila mwezi kugharamia mahitaji ya mwanawe.

Mama huyo anaomba korti iamuru awe akipewa Sh50,000 za ada ya nyumba, Sh35,000 za matibabu, mshahara wa mjakazi Sh15,000, maankuli Sh35,000, nguo Sh40,000 na ada ya starehe Sh35,000 kila mwezi.

Mama huyo ameeleza mahakama, mshtakiwa hupokea mshahara mnono. Katika ushahidi wake wa kujitetea aliowasilisha mahakamani, Bw Shinali , ameyakana madai kwamba alimpachika mimba , Mutheu kama anavyodai.

“Mimi siyajui kamwe madai kuwa mimi ndiye baba wa mvulana huyo,” Bw Shinali ameeleza katika ushahidi wake kwa mahakama.

Kesi hiyo ilipowasilishwa, Bw Shinali alikataa kata katu kwamba alimzaa mtoto huyo na kuomba mahakama iamuru uchunguzi zaidi ufanywe kubaini madai ya mwanamke huyo.

Mahakama iliamuru uchunguzi wa DNA ufanywe ndipo ukweli ujulikane uwongo ujitenge. Mahakama inayochunguza kesi hiyo iliamuru mnamo Machi 2020 uchunguzi wa DNA ufanywe.

Bw Shinali aliomba kesi isitishwe kusubiri matokeo ya uchunguzi wa DNA kutoka kwa maabara ya Serikali.

Sampuli za kufanyiwa uchunguzi wa maabara zilitwaliwa kutoka kwa Bw Shinani , Mutheu na mwanaye kukaguliwa kiutalaamu wa kisayansi kubaini uzazi wa mtoto huyo.

Mkaguzi katika maabara ya Serikali Bi Pamela Khamala Okelo alipokea sampuli hizo na kuzikagua kwa makini. Uamuzi uliofikiwa katika maabara hiyo ya Serikali na kuwasilishwa kortini ulibaini kuwa Bw Shinali ndiye baba wa mtoto huyo.

“Kulingana na uchunguzi uliofanyiwa sampuli zilizopokewa katika maabara ya Serikali imebainika kwa asilimia 99.99 Bw Bernard Masaka Shinali ndiye baba mzazi wa mtoto wa Caroline Mutheu,” Bi Okelo amesema katika ripoti aliyoiwasilisha kortini mnamo Aprili 7, 2020.

Katika ushahidi wake, Mutheu ameeleza kuwa mnamo Mei 7,2016 walimzaa mwanaye baada ya “ mapenzi kunoga baina yao.”

Lakini ameeleza kuwa, mbunge huyo hawasaidii yeye na mwanawe na “hata hajui tunachokula, kunywa na hata makazi yetu yako na shida.”

Mutheu anaomba mahakama iamuru Bw Shinali awe akigharamia , matibabu ,chakula, makazi, gharama za hospitali na elimu ya mwanaye.

“Mshtakiwa (shinali) ni Mbunge wa Ikolomani iliyoko kaunti ya Kakamega na hupata ndonge nono kila mwezi,” asema Mutheu katika hati zake za ushahidi mahakamani.

Mlalamishi huyo anasema kuwa ndiye anayegharamia mahitaji ya mwanaye na yuahiti “fedha sisizo haba kugharamia mahitaji yake.“

Mutheu amesema mtoto huyo anahitaji maisha mazuri na endapo “ Bw Shinali hatashurutishwa na mahakama kugharamia mahitaji ya mtoto huyo bila shaka ataanza kuishi maisha ya uchochole.”

Mutheu anaomba korti isimame kidete na kuamuru haki za mtoto huyo zilindwe na apewe kile anachohitaji kukua na kuishi maisha yasiokumbwa na bughudha.

Pia anaomba mahakama ipitisha maagizo mengine inayoona yanamfaa , mtoto huyo. Kesi itasikizwa Machi 9,2021.

You can share this post!

Wanaoendeleza ukeketaji Lamu wazimwa

Unayostahili kufanya ili kujikinga na ugonjwa wa moyo