• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Raila atua Pwani kufunza wakazi kusakata Reggae

Raila atua Pwani kufunza wakazi kusakata Reggae

KIONGOZI wa Chama cha ODM, Raila Odinga leo amepangiwa kuanza rasmi ziara yake eneo la Pwani kupigia debe mswada wa marekebisho ya katiba kupitia Mpango wa Maridhiano (BBI).

Bw Odinga jana alitua katika Kaunti ya Taita Taveta lakini hakufanya mkutano wowote wa hadhara ilivyotarajiwa na wengi.Amepangiwa kuzuru kaunti za Mombasa, Kwale, Kilifi, Lamu na Tana River ili kuendeleza kampeni za BBI katika ukanda huo.

Bw Odinga leo amepangiwa kukagua soko la kisasa la Mwatate, mradi wa ujenzi wa hospitali ya ugonjwa wa corona mjini humo kisha kuhutubia wenyeji wa mji huo kabla ya kufungua shule ya Mwakinyungu katika eneo la Rong’e.

Baadaye atahutubia wenyeji wa Voi kabla ya kuendeleza safari yake Kaunti ya Mombasa.’Safari yake inalenga kuzindua kampeni za BBI katika eneo la Pwani,’ alisema mwenyekiti wa ODM katika Kaunti ya Taita Taveta, Richard Tairo.

Kiongozi huyo pia atakutana na viongozi wa kaunti hiyo ili kujadili mikakati ya kuendeleza kampeni za BBI katika eneo hilo.Baadhi ya viongozi wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano huo ni gavana Granton Samboja, seneta wa kaunti hiyo Jones Mwaruma, wabunge Jones Mlolwa (Voi), Andrew Mwadime (Mwatate), aliyekuwa mbunge wa Wundanyi Thomas Mwadeghu na madiwani.

Vilevile ziara ya kiongozi huyo inapania kufufua umaarufu wake unaotishiwa kudidimia viongozi wengi wakipigania chama huru cha Wapwani.

Chama cha ODM, ambacho kimekuwa kikipata uungwaji mkono mkubwa katika eneo hilo, kilipata pigo baada ya baadhi ya wanasiasa kuhamia mrengo wa Tangatanga unaounga mkono azma ya Naibu Rais William Ruto.

Viongozi hao vilevile wamekuwa mstari wa mbele kupinga BBI na hivyo kuzua tumbojoto ikiwa mswada huo utapenya ifikapo kura ya maoni mnamo Juni.

Ziara ya kiongozi huyo inajiri baada ya Dkt Ruto kuzuru eneo hilo wiki chache zilizopita. Bw Raila ananuia kupoza ziara ya Bw Ruto ambaye anaaminika kuwa anaendelea kupata umaarufu katika eneo hilo.

You can share this post!

Chaguzi ndogo kuamua vigogo wa siasa Magharibi

Duale azimwa kuandaa mswada wa kuzima ngono mitandaoni