Na SAMMY WAWERU
MBUNGE wa Ruiru Bw Simon King’ara ameahidi wahudumu wa tuktuk na magari madogo aina ya maruti eneo la Githurai 45 kwamba atawasaidia kuimarisha hali ya usalama.
Wahudumu hao wamekuwa wakilalamikia usalama kudorora katika utendakazi wao. Visa vya magari hayo ya usafiri na uchukuzi kuibwa vimekuwa vikiripotiwa.
Vilevile, wahudumu hao wamekuwa wakiteta sehemu muhimu ya magari yao kama vile magurudumu na betri kutolewa.
“Ushirikiano ni jambo la muhimu katika utendakazi, tutashirikiana kuhakikisha usalama katika sekta ya tuktuk umeimarika,” Bw King’ara akasema.
Mtaa wa Githurai 45 uko katika eneobunge la Ruiru, na mbunge huyo pia aliahidi kusaidia kuimarisha hali ya barabara eneo hilo.
Bw King’ara alisema hayo baada ya kukutana na viongozi wa muungano wa wamiliki wa tuktuk na maruti (GTMA), waliochaguliwa kufuatia uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa juma lililopita.
“Ninaelewa hali ya baadhi ya barabara Githurai si bora. Tutaziimarisha kufuatia mradi wa ukarabati unaoendelea,” akasema.
Barabara inayounganisha mtaa wa Githurai na Mwihoko, inaendelea kuwa mbovu, mashimo yakizidi kushuhudiwa.