• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Raila awaonya Wapwani dhidi ya kuunda chama

Raila awaonya Wapwani dhidi ya kuunda chama

LUCY MKANYIKA na MAUREEN ONGALA

KIONGOZI wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga, amepinga msukumo wa baadhi ya viongozi wa Pwani kuunda chama cha kisiasa cha kutetea maslahi ya eneo hilo.

Akizungumza katika Kaunti ya Taita Taveta alipoanza ziara ya kuvumisha pendekezo la kurekebisha katiba kupitia Mpango wa Maridhiano (BBI), Bw Odinga alisema pendekezo la kuunda chama cha ukanda huo kitaleta mgawanyiko wa nchi.

Wito wa uundaji chama cha Wapwani umekuwa ukivumishwa na viongozi wengi katika ukanda wa Pwani.

Hata hivyo, katika wiki chache zilizopita, wengi wao waliachana na mipango hiyo ambayo sasa inaonekana kuendelezwa na Gavana wa Kilifi, Bw Amason Kingi na wandani wake pekee.

Bw Odinga alisema kuwa katiba inawapa Wakenya haki ya kuunga mkono mrengo wowote bila kueneza ukabila nchini.Viongozi wanaoegemea upande wa Naibu Rais William Ruto katika ukanda huo walitangaza wataingia katika Chama cha United Democratic Alliance badala ya kuendeleza mipango ya awali ya kuunda chama cha Wapwani.

Kwa upande mwingine, Gavana wa Mombasa, Bw Hassan Joho alisema aliwekeza sana katika uundaji wa chama cha ODM kwa hivyo hana nia ya kukihama chama hicho kwa sasa, anapolenga kutafuta tiketi yake kuwania urais 2022.

Bw Odinga alionya kuwa, kutakuwa na hatari ya kusababisha migawanyiko endapo viongozi wa Pwani wataunda chama ambacho hakitakuwa na mtazamo wa kitaifa.

“Katika katiba, Kenya ni demokrasia ya vyama vingi na tunataka kuwa na vyama vya kitaifa. Tukianza kuwa na vyama vya majimbo, tutagawanya Kenya. Kama unataka kuunda chama, katiba haikuruhusu kuanzisha chama cha ukoo au kikabila. Huo ni ushauri ningetaka kuwapa watu wa Pwani,” akasema.

Hapo jana, balozi huyo wa miundomsingi katika Muungano wa Afrika (AU), alifanya mikutano mbalimbali Kaunti ya Taita Taveta.Alikuwa ameandamana na viongozi wa eneo hilo wakiongozwa na Gavana Granton Samboja.

Katika mikutano ya hadhara, viongozi waliohutubu waliahidi wananchi kwamba mswada wa BBI ukipitishwa utaleta manufaa kwa maendeleo na uongozi bora.

Kulingana nao, mapendekezo kama vile kuongeza mgao wa fedha kwa kaunti na kutengea madiwani pesa za maendeleo ya wadi, yatasaidia kustawisha nchi katika maeneo ya mashinani.Msafara wa Bw Odinga leo umepangiwa kuelekea Kaunti ya Kilifi ambayo imegeuka kitovu cha wito wa uundaji chama cha Wapwani.

Mbunge wa Ganze, Bw Teddy Mwambire, alisema kuwa ziara ya Bw Odinga haihusu masuala ya chama bali BBI.Jumatatu wabunge wa chama ODM Kaunti ya Kilifi pamoja na wajumbe wa Kaunti hiyo walifanya kikao kirefu na Bw Kingi kujiandaa kwa ziara ya Bw Odinga.

 

You can share this post!

Marseille wamfuta kazi kocha Villas-Boas na kumwajiri Jorge...

Mwanamke adai Mungu alimtuma kumumunya Sh30 milioni katika...