• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Wanahabari wataka waorodheshwe kwa watakaopewa chanjo ya corona

Wanahabari wataka waorodheshwe kwa watakaopewa chanjo ya corona

Na CHARLES WASONGA

CHAMA cha kutetea masilahi ya Wanahabari Nchini (KUJ) sasa anaitaka serikali kujumuisha wanachama wake miongoni mwa wafanyakazi watakaopewa chanjo ya corona kwanza.

Kwenye taarifa, Katibu Mkuu wa chama hicho Eric Oduor alilalama kuwa mwongozo wa utoaji chanjo ya Covid-19 haujaorodhesha wanahabari kama wa kwanza kupewa chanjo hiyo.

“KUJ inataka wanahabari wajumuishwe kwenye orodha ya wafanyakazi ambao watapewa kipaumbele na kuwa wa kwanza kupewa chanjo ya corona inayowasilishwa nchini wiki hii,” akasema.

Bw Oduor pia alimtaka Waziri wa Afya Mutahi Kagwe kutambua vyombo vya habari kama asasi muhimu katika kampeni ya kitaifa ya kupambana na Covid-19.

Kauli ya KUJ inajiri kufuatia tangazo la Wizara ya Afya kwamba wahudumu wa afya, walinda usalama na walimu ndio wafanyakazi ambao watapewa chanjo hiyo kwanza. Hii ni kutoka na majukumu yao ambayo yanawafanya kutangama na wananchi na hivyo kuwaweka katika hatari ya kuambukizwa virusi vya corona.

Kenya itapokea shehena ya kwanza ya dozi 1.02 milioni ya chanjo aina ya AstraZeneca kutoka Uingereza mnamo Jumanne usiku. Hii ni sehemu ya dozi au vipimo 4.1 milioni ambayo Kenya inatarajia kupokea na kusambaza katika awamu ya kwanza ya usambazaji chanjo hiyo ambayo ni kati ya mwezi Machi hadi Juni.

KUJ sasa inasisitiza kuwa wanahabari wanafaa kuwa miongoni mwa wafanyakazi wa kupewa chanjo hiyo kwa sababu kazi yao inawalazimu kutagusana na wananchi kila siku na hivyo kuwaweka katika hatari ya kuambukizwa Covid-19.

“Wanahabari pia wanafaa kukingwa dhidi ya corona. Inasikitisha kuwa hawajajumuishwa miongoni mwa wafanyakazi walioko mstari wa mbele kupewa chanjo. Isiwe kwamba wanahabari ni muhimu tu nyakati za dharura wakati ambapo huduma zao zinahitajika lakini masilahi yao hayathaminiwi,” akalalama Bw Odour.

Tangu kisa cha kwanza cha Covid-19 kuripotiwa nchini mnamo Machi 13, 2020, wanahabari ni miongoni mwa wale ambao wameambukizwa vizuri corona vinavyosababisha homa hiyo hatari.

Mwaka jana, Rais Uhuru Kenyatta alipotangaza mwongozo kuhusu udhibiti wa Covid-19, wanahabari waliorodheshwa miongoni mwa makundi 13 ya wafanyakazi wanaotoa hudumu muhimu na ambao wanafaa kusazwa wakati wa utekelezaji wa kafyu.

You can share this post!

Taharuki kuhusu teknolojia ya kutambulisha nyuso

Morans yaimarika kwenye viwango bora vya mpira wa vikapu...