• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Mwaniaji wa udiwani wa UDA akamatwa kwa kuhonga wapigakura

Mwaniaji wa udiwani wa UDA akamatwa kwa kuhonga wapigakura

RUTH MBULA Na SAMMY WAWERUUDA

MAAFISA wa polisi katika Kaunti ya Kisii walimtia nguvuni mgombea wa kiti cha udiwani kwa tiketi ya chama cha UDA, mapema Alhamisi kufuatia uchaguzi mdogo unaofanyika wadi ya Kiamokama.

Bw Moses Nyandusi Nyakeremba alikamatwa kutokana na madai ya kuhonga wapiga kura, katika eneo la Moremani.

Mwanasiasa tajika Don Bosco Gichana, ambaye ni mfuasi wa UDA pamoja na wafuasi wengine pia walitiwa nguvuni.

Wapiga kura walianza kumiminika vituoni mwendo wa saa kumi na mbili za asubuhi, foleni ndefu zikishuhudiwa katika vingi vya vituo.

Afisa rejeshi wa tume huru ya uchaguzi na mipaka (IEBC) Kiamokama, Bw Mark Manco alisema wadi hiyo ina vituo 22 vya kupigia kura, na jumla ya wapiga kura 10, 853 wliosajiliwa.

Kwa muda wa wiki kadha zilizopita, kundi la Tangatanga, chini ya mrengo tawala wa Jubilee na vilevile chama cha ODM, wafuasi wamekuwa wakiendesha kampeni kutafutia wagombea wao kura.

Gavana wa Kisii Bw James Ongwae, Seneta Prof Sam Ongeri, mbunge Mwakilishi wa Wanawake kaunti hiyo, Bi Janet Ongera na mbunge wa Dagoreti Kaskazini, Simba Arati, wamekuwa wakifanyia kampeni mwaniaji wa ODM, Bw Malack Matara.

Nalo kundi la Tangatanga, likiongozwa na Niabu Gavana wa Kisii, Bw Joash Maangi, aliyekuwa mwenyekiti wa tume ya utekelezaji Katiba Bw Charles Nyachae na kiongozi wa PDP Bw Omingo Magara walipigia debe mgombea wao, Bw Moses Nyakeramba.

Wabunge wengine wa Tangatanga ambao wamekuwa wakisaidia mwaniaji huyo kusaka kura ni pamoja na Mabw Silvanus Osoro (Mugirango Kusini) na Alpha Miruka (Bomachoge Chache).

Kundi hilo linahusishwa na Naibu wa Rais, Dkt William Ruto.

Tangatanga iliamua kuunga mkono Bw Nyakeramba baada ya kufanya mkutano na Dkt Ruto, nyumbani kwake eneo la Karen, Nairobi.

Hatua ya Naibu wa Rais kuunga mkono mgombea huyo wa kiti cha udiwani Kiamokama kwa tiketi ya UDA, inalenga kuvumisha umaarufu wake katika jamii ya Abagusii.

“Ni kweli tulikutana na Naibu wa Rais, tukaafikiana kuunga mkono Bw Nyandusi Nyakeramba kama mgombea wa Tangatanga. Hatua hiyo imeondoa shauku kati yetu, ni nani tutaunga mkono,” Bw Maangi akasema.

Awali, Bw Nyandusi, ambaye alikuwa akihudumu kama mkurugenzi mkuu wa kampuni ya majanichai, alikuwa katika njiapanda kufuatia kutoelewana kwa wandani wa Dkt Ruto Kisii ni nani wangeunga mkono.

Waliafikiana kumuunga mkono juma moja kabla ya uchaguzi huo mdogo, na baada ya kufanya kikao na Naibu Rais.

IEBC iliratibu uchaguzi huo kufanyika, Machi 4, 2021 na kuidhinisha wagombea 11.

Kiti cha udiwani Kiamokama kilisalia wazi kutokana na kifo cha aliyekuwa diwani, Bw Kennedy Mainya, mnamo Novemba 2020.

Bw Daniel Ondabu na ambaye amewahi kuwa mtumishi wa umma ndiye mgombea wa kiti hicho kwa tiketi ya chama kipya cha PED.

“Tuna imani kushinda na kutwaa kiti hiki,” Katibu Mkuu wa PED, Bw Enock Ombuna akaambia Taifa Leo Dijitali.

Wawaniaji wengine ni pamoja na Bw Adams Nyamori Nyakundi (Maendeleo Chap Chap), Stephen Nyakeriga (TND), Dkt Charles Omwega (PEP), Dominic Ateng’a Nyangaresi (KNC), Peter Mwaboto (Narc-Kenya) na mwanaharakati Vincent Gekone kama mgombea wa kujitegemea.

Chama cha ODM kinatetea kuhifadhi kiti hicho kupitia mgombea wake, Malack Matara.

You can share this post!

Kiunjuri abadilisha wimbo, sasa asakata Reggae ya BBI

Wabunge 4 wa Tangatanga wakamatwa kwa kuhonga wapigakura