• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Mwandishi wa NMG, Pauline Ongaji atuzwa

Mwandishi wa NMG, Pauline Ongaji atuzwa

NA RICHARD MAOSI

MWANDISHI wa masuala ya afya na mazingira katika kampuni ya Nation Media Group (NMG) Bi Pauline Ongaji ametajwa kama mwanahabari bora zaidi katika uandishi wa makala ya kuzuia maradhi yasiyoambukizwa, katika tuzo za kwanza za Afrika Mashariki kwa Wanahabari wanaoripoti masuala hayo.

Akiwa na tajriba ya miaka kumi katika uanahabari, Bi Ongaji amejizolea umaarufu kote nchini kwa makala yake yenye mvuto wa kipekee yanayochapishwa na magazeti ya Taifa Leo, Daily Nation na Business Daily.

Akiashiria furaha yake baada ya kutuzwa katika hafla iliyoandaliwa jijini Kampala, Uganda hapo Ijumaa, Bi Ongaji alisema kuwa juhudi zake zimepata tuzo inayostahili baada ya miaka mingi ya kuandika makala yanayobadilisha jamii.

“Ninaona fahari kutambuliwa na shirika la hadhi kama hili. Furaha yangu inatokana na jinsi makala yangu yamesaidia mamilioni ya watu kwa lugha ya Kiingereza na Kiswahili hapa Afrika Mashariki,” aliambia Taifa Leo Dijitali.

Baadhi ya makala yaliyomshindia mwanahabari huyo tuzo hiyo ni ‘Kansa ya lango la uzazi bado changamoto mashambani’ iliyochapishwa na Taifa Leo, ‘When you get a donor but you can’t get treatment’ iliyochapishwa na Daily Nation na ‘Kidney patients grapple with transplant queues headache’ iliyotokea katika Business Daily.

“Nyakati zote mimi husafiri hadi mahali ambapo habari zinatendeka ili kupata hisia za waathiriwa. Lengo langu ni kuonyesha jinsi magonjwa haya yanaathiri jamii mbalimbali na suluhu zilizopo.”

Mamia ya wanahabari kutoka Kenya, Uganda, Tanzania, Zanzibar, Rwanda na Burundi walishiriki katika tuzo hizo ambazo ziliangazia makala yaliyofanyiwa utafiti wa kina na kuandikwa kwa lugha ya kipekee.

“Tulikuwa tunawazawidi wale ambao wameandika makala yaliyochanganuliwa vizuri. Pia tulitaka kuwatambua wanahabari wenye talanta ya kuandika habari kwa lugha rahisi, yenye mvuto mkuu na inayoeleweka na wasomaji wa jamii mbalimbali,” akasema Proscovia Nabatte, mratibu wa tuzo hizo.

You can share this post!

‘Tuliangusha BBI kuadhibu gavana’

Dkt Patrick Amoth Mkenya wa kwanza kupata chanjo ya corona