• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 9:55 AM
Mpango wa kusafisha Pwani wazinduliwa

Mpango wa kusafisha Pwani wazinduliwa

Na WANDERI KAMAU

SHIRIKA la Petco Kenya na Hazina ya Kuhifadhi Mazingira (WWF) zimetia saini mkataba wa Sh6 milioni, kuimarisha juhudi za kuhifadhi mazingira na uzoaji taka katika ukanda wa Pwani.

Mkataba huo utayawezesha mashirika hayo kupata mashine maalum ya kuboresha taka kupitia teknolojia ya kisasa kutoka Denmark.Mpango huo utaendeshwa kwa ushirikiano na kampuni ya Plastix kutoka taifa hilo, ambayo hujihusisha na kuboresha taka.

Kaunti zinazolengwa kwenye mkakati huo ni Kwale, Mombasa, Kilifi na Lamu.Hilo pia litaendeshwa kwa kuyashirikisha mashirika mengine nchini ambayo yamekuwa yakijihusisha na shughuli za uzoaji taka.

Kulingana na Msimamizi Mkuu wa shirika la Petco nchini, Bi Joyce Gachugi, lengo kuu la mpango huo ni kuimarisha shughuli za uzoaji taka nchini, na kuzigeuza kwa namna zinazoweza kuifaidi jamii.

“Lengo letu ni kuondoa taka aina ya plastiki katika ukanda wa Pwani, kubuni mazingira bora ya kufanyia kazi na kuunga mkono juhudi zinazoendeshwa na wakfu wa WWF katika kusafisha miji, bandari na mito. Mpango huu ni muhimu sana kwetu kwani unapiga jeki juhudi zetu kuwasaidia kifedha watu binafsi na mashirika ambayo yamekuwa yakijihusisha katika uzoaji taka,” akasema.

Mpango pia unalenga kutoa mashine maalum za uzoaji taka na mafunzo maalum kwa zaidi ya watu 800 ambao wamekuwa wakijihusisha katika shughuli hizo.

Mchakato huo mzima utagharimu Sh 6 milioni.Ripoti mbalimbali zimeiorodhesha Pwani kuwa miongoni mwa maeneo yanayokusanya kiwango kikubwa zaidi cha taka nchini.

Taka nyingi huwa vifaa vinavyotengenezwa kwa plastiki.Maeneo ambayo yamekuwa yakiathiriwa sana na tatizo hilo ni fuo za Bahari Hindi, hali ambayo wanamazingira wametaja kuhatarisha maisha ya viumbe wa majini kama samaki.

Wanaharakati wa mazingira wamekuwa wakiwalaumu viongozi wa kisiasa kwa kutolichukulia suala hilo kwa uzito.Wasimamizi wa mkakati huo walisema wanalenga kuchangia katika juhudi za kuendeleza maendeleo endelevu na kuboresha maisha ya wanawake na wanaume, hasa vijana.

Hili ni kwa kugeuza uzoaji taka kuwa kazi wanayoweza kuifanya kuwa biashara ili kujipatia mapato maishani.Juhudi vile vile zinalenga kuchochea uvumbuzi na kubuni soko la uboreshaji taka.Baadhi ya mashirika yatakayoshirikishwa kwenye mkakati huo ni Plastix, Jil Plastics na Kwale Plastic Plus Collectors (KPPC).

Mashirika hayo yaliungana na kuanza juhudi za kukabili athari za uharibifu wa mazingira unaochangiwa na vifaa vya plastiki katika ukanda huo.Msimamizi Mkuu wa Miradi ya Uhifadhi katika WWF, Bi Nancy Githaiga, alisema kupitia juhudi hizo, wanalenga kubuni ushirikiano wa kimataifa utakaochangia pakubwa katika kuhakikisha uzoaji taka umegeuzwa kuwa mfumo wa kimapato kwa maelfu ya watu.

You can share this post!

Hatimaye Echesa atiwa nguvuni

Wapwani wataka kummeza Yatani kuhusu Bandari